Kocha Mkuu wa Yanga Romain Folz amesema ana imani na mshambuliaji Prince Dube licha ya kukosa nafasi nyingi katika mchezo wa mkondo wa kwanza hatua ya awali ligi ya mabingwa dhidi ya Wiliete SC
Kesho Jumamosi Yanga itakuwa mwenyeji wa Wiliete SC katika uwanja wa Benjamin Mkapa ikiwa kifua mbele kufuatia ushindi wa mabao 3-0 katika mchezo wa kwanza uliopigwa Angola
Dube alikuwa miongoni mwa wafungaji katika mchezo huo ambao Aziz Andabwile na Edmund John pia walifunga mabao. Dube pia alipoteza nafasi kadhaa za wazi na kuibua mijadala katika mitandao ya kijamii
Folz amesema ana imani na mshambuliaji huyo raia wa Zimbabwe na ndio maana aliendelea kumuacha dimbani katika mchezo huo na hatimaye akafunga
Folz raia wa Ufaransa amesema jambo muhimu kwa timu yake kwa sasa ni kuwa wanatengeneza nafasi nyingi ingawa bado ufanisi wao sio mzuri sana na hivyo ataendelea kufanyia kazi mapungufu hayo katika uwanja wa mazoezi
"Bado hatuko katika changamoto kubwa ingawa ni kweli ufanisi wetu katika matumizi ya nafasi hauridhishi, tutaendelea kufanya kazi katika uwanja wa mazoezi ili tuboreshe"
"Lakini lazima niwaamini wachezaji wangu pale ninapowapa majukumu. Mfano Prince Dube alipoteza baadhi ya nafasi za wazi katika mchezo uliopita Angola, niliendelea kumuacha uwanjani kwa sababu namuamini"
"Na imani hiyo ilileta matunda kwani aliweza kufunga baadae, Sasa kama ningemtoa labda dakika ya 60 pengine mambo yangeweza kuwa tofauti"
"Tunatengeneza nafasi nyingi ni kweli, lakini pia tunafunga mabao kupitia nafasi hizo, tutaendelea kufanya kazi kwenye uwanja wa mazoezi ili tuongeze ufanisi zaidi mbele ya lango," alisema Folz



