Uongozi wa klabu ya Simba utalazimika kuamua hatma ya kiungo mshambuliaji Jean Charles Ahoua katika dirisha hilo baada ya kupokea ofa kadhaa kwa ajili yake, imefahamika.
Ahoua bado ana mkataba na Simba hadi mwisho wa msimu lakini inaelezwa kuna ofa nono kutoka Arabuni na pia Raca CA ya Morocco.
Kocha wa Raja CA Fadlu Davids anapambana kumnasa kiungo huyo mshambuliaji ambaye unaweza kusema alibeba ramani yake ya mafanikio akiwa na Simba kabla ya kutimkia Morocco mwanzoni mwa msimu huu.
Mpaka sasa hakuna mazungumzo ya kuongeza mkataba wake na pengine Simba inaweza kumpoteza akiwa mchezaji huru kama watasubiri mkataba wake umalizike.
Kocha mpya wa Simba Steve Barker anamuona Ahoua kama mchezaji muhimu katika kikosi chake akihitaji kuendelea kuwa nae.
Hivyo mtihani umebaki kwa mabosi wa Simba ambao wanapaswa kuamua sasa wachukue pesa au waendelee kumshawishi aongeze mkataba mpya.