Klabu ya Simba imemrejesha kiungo fundi raia wa Zambia, Clatous Chama ‘Mwamba wa Lusaka’, hatua iliyozua mjadala mkubwa miongoni mwa wadau wa soka nchini kutokana na mchango mkubwa aliowahi kuutoa ndani ya kikosi hicho.
Chama, ambaye alitua kwa mara ya kwanza Simba mwaka 2018 akitokea Lusaka Dynamos ya Zambia, aliitumikia klabu hiyo kwa mafanikio kabla ya kuondoka Agosti 2021 alipouzwa kwenda RS Berkane ya Morocco. Hata hivyo, hakudumu sana na Wamorocco hao na kurejea Simba Januari 2022.
Baada ya kumaliza mkataba wake Julai 2024, kiungo huyo alijiunga na Yanga kwa msimu mmoja wa 2024–2025, kisha Septemba 2025 akasajiliwa na Singida Black Stars kabla ya kurejea tena Simba Januari 2026.
Uamuzi wa Simba kumrudisha Chama umechangiwa kwa kiasi kikubwa na biashara ya kumuuza kiungo Jean Charles Ahoua, ambaye alihamia CR Belouzdad ya Algeria dirisha hili la usajili.
Ahoua alikuwa mhimili muhimu msimu uliopita akifunga mabao 16 na kutoa pasi tisa za mabao, huku akiisaidia Simba kufika fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu wa 2024–2025.
Kuondoka kwa Ahoua kumeacha pengo kubwa katika eneo la kiungo mshambuliaji, nafasi ambayo sasa inatarajiwa kuzibwa na Chama. Kiungo huyo anarejea akiwa na kumbukumbu nzuri ndani ya Simba, akihusika moja kwa moja katika mabao 102 (asisti 60 na mabao 42) ndani ya mechi 183 alizocheza Ligi Kuu Bara na mashindano ya kimataifa.
Mbali na uzoefu wake wa ndani, Chama amedhihirisha ubora wake pia katika klabu alizopita. Akiwa Singida Black Stars, alitoa mchango mkubwa katika safari ya klabu hiyo kufuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika kwa kuwaondoa Rayon Sports ya Rwanda kwa jumla ya mabao 3-1 na Flambeau du Centre ya Burundi kwa jumla ya mabao 4-2. Kati ya mabao saba yaliyofungwa na Singida, Chama alihusika katika matatu kwa kufunga mawili na kutoa asisti moja.
Msimu huu, Chama amefunga mabao sita katika mashindano mbalimbali, yakiwemo matatu ya Kombe la Kagame ambapo aliibuka mfungaji bora, jambo linaloonyesha kuwa bado ana makali ya kufumania nyavu licha ya kucheza nafasi ya kiungo.
Urejeo wa Chama unakuja wakati Simba ikijiandaa na mchezo mgumu wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Esperance ya Tunisia utakaochezwa Januari 24, 2026. Uzoefu wake wa mechi za kimataifa unatajwa kuwa silaha muhimu kwa kikosi hicho katika pambano hilo la ugenini.
Kwa ujumla, kurejea kwa Clatous Chama kunatarajiwa kuiongezea Simba ubunifu katikati ya uwanja, mabao kutoka safu ya pili pamoja na uongozi wa ndani ya uwanja.
Ikiwa atapata nafasi ya kucheza kikosi cha kwanza, mashabiki wa Simba wana kila sababu ya kuamini kuwa Mwamba wa Lusaka anaweza kuendeleza pale alipoishia na kuisaidia klabu yao kufikia malengo ya msimu huu wa ndani na kimataifa.



