Azam FC imefufua rasmi matumaini ya kusonga mbele katika Kombe la Shirikisho Afrika (CAFCC) baada ya kupata ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Nairobi United katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Nyayo, jijini Nairobi, Kenya.
Mchezo ulianza kwa presha kubwa kutoka kwa wenyeji Nairobi United, waliotumia vyema uwanja wao wa nyumbani na kushangilia bao la mapema dakika ya 15 kupitia kwa Dancun Oluoch. Bao hilo liliwapa morali kubwa mashabiki wa Nairobi United waliokuwa wakitarajia ushindi wa kwanza nyumbani katika michuano hiyo.
Hata hivyo, Azam FC hawakukata tamaa. Dakika mbili tu baadaye, dakika ya 17, mshambuliaji Japhte Kitambala aliisawazishia Azam FC kwa bao zuri lililorejesha matumaini na kuibadilisha kabisa mwelekeo wa mchezo. Bao hilo liliwafanya wachezaji wa Azam FC kujiamini zaidi na kuanza kudhibiti mchezo, hasa katikati ya uwanja.
Kipindi cha pili kilikuwa na ushindani mkubwa huku kila timu ikitafuta bao la ushindi. Dakika ya 78, presha ya Azam FC ilizaa matunda baada ya Nairobi United kujifunga bao la kujitakia, bao lililovunja kabisa matumaini ya wenyeji kuokota alama kwa mara ya kwanza wakiwa nyumbani katika mashindano hayo.
Ushindi huu ni wa kwanza kwa Azam FC katika michuano ya CAFCC msimu huu, baada ya kupoteza mechi mbili za awali katika hatua ya makundi. Matokeo haya yanaipa Azam FC pointi muhimu na kufufua matumaini ya kusonga mbele kuelekea hatua ya robo fainali, huku yakiongeza morali kwa kikosi na benchi la ufundi kabla ya michezo ijayo.
Kwa ushindi huu wa ugenini, Azam FC wamethibitisha kuwa bado wana nafasi ya kupambana na kurejesha heshima yao katika michuano ya kimataifa, jambo linalowapa mashabiki wao sababu mpya ya kuamini na kuendelea kuiunga mkono timu yao.
Wawakilishi wengine wa Tanzani katika michuano hiyo Singida BS wamepata ushndi muhimu wa bao 1-0 dhidi ya Otoho katika mchezo uliopigwa uwanja wa New Amaan Complex.
Bao pekee la Singida BS katika mchezo huo lilifungwa na Elvis Rupia