Kiungo mshambuliaji wa klabu ya Young Africans SC, Celestin Ecua, amekamilisha rasmi uhamisho wake wa mkopo kwenda klabu ya JS Kabylie ya Algeria, katika hatua inayohitimisha safari yake ya muda mfupi ndani ya kikosi cha Wananchi.
Ecua ametua Algeria kwa mkopo wa mwaka mmoja, baada ya Yanga kufanya maamuzi ya kumwondoa kwenye mipango ya kikosi cha msimu huu, huku klabu ikichagua kufanya maboresho makubwa kupitia dirisha dogo la usajili.
Awali, nyota huyo alikuwa akihusishwa na uhamisho kwenda Sekhukhune United ya Afrika Kusini, sambamba na kiungo mwingine Mohamed Doumbia, ambaye naye pia hakuwa sehemu ya mipango ya kocha wa Yanga.
Hata hivyo, JS Kabylie imeibuka kuwa kituo kipya cha Ecua, ikimpa nafasi ya kuendeleza kipaji chake kwenye moja ya ligi zenye ushindani mkubwa barani Afrika.
Hatua ya Yanga kumuacha Ecua inakuja baada ya klabu hiyo kuongeza nguvu mpya kupitia usajili wa wachezaji watatu wa kigeni kwenye dirisha dogo, ambao ni Depu, Allan Okello na Yao Kouassi. Sambamba na hilo, Wananchi wameamua kuachana na baadhi ya wachezaji wa kigeni akiwemo And Boyeli, Mohamed Doumbia na sasa Celestin Ecua.



