Klabu ya Simba SC imeendelea kuonyesha dhamira yake ya kuimarisha kikosi chake kwa kukamilisha usajili wa kiungo mshambuliaji Inno Jospin Loemba (21) kutoka klabu ya Colombe Sports ya Cameroon.
Loemba tayari ametua jijini Dar es Salaam, hatua inayofungua ukurasa mpya katika safari yake ya soka barani Afrika Mashariki.
Taarifa kutoka ndani ya klabu zinaeleza kuwa huenda utambulisho wake ukafanyika leo, kabla ya kujiunga moja kwa moja na kikosi cha Simba kinachorejea mazoezini kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Mashujaa FC, unaotarajiwa kuchezwa siku ya Alhamisi.
Usajili wa Loemba unakuja katika kipindi muhimu kwa Simba, ambayo ina ratiba ngumu ya michezo. Baada ya pambano dhidi ya Mashujaa FC, wekundu wa Msimbazi wanatarajiwa kurejea mawindoni kimataifa, wakiweka nguvu zao kwenye mchezo mkubwa dhidi ya Esperance de Tunis, utakaopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa siku ya Jumapili.
Licha ya kusajiliwa kutoka klabu ya Cameroon, Loemba ni raia wa Congo Brazzaville, na amekuwa mmoja wa wachezaji muhimu wa Colombe Sports, ambapo aliwahi pia kuwa nahodha wa kikosi hicho ishara ya uwezo wake wa uongozi na uzoefu uwanjani licha ya umri wake mdogo.






