Hatma ya beki wa kulia wa Real Madrid na timu ya taifa ya England, Trent Alexander-Arnold (27), inaendelea kuwa gumzo barani Ulaya, huku nyota huyo akiripotiwa kukumbana na changamoto kubwa ndani ya kikosi cha Los Blancos tangu kuanza kwa dirisha la usajili la majira haya ya kiangazi.
Taarifa zinaeleza kuwa Manchester City inaendelea kumfuatilia kwa karibu Trent, ikivutiwa zaidi na uwezo wake wa kupandisha mashambulizi, kutoa pasi za mwisho na kusoma mchezo kwa haraka. Mabingwa hao wa England wanaamini kuwa wanaweza kuipata saini yake iwapo watawasilisha ofa nono kwa Real Madrid.
Trent amekuwa akihusishwa na nia ya kuondoka BernabΓ©u, kufuatia kushindwa kujihakikishia nafasi ya kudumu katika kikosi cha kwanza. Licha ya kurejea uwanjani baada ya kusumbuliwa na majeraha ya mara kwa mara, kiwango chake kimeelezwa kutokuwa cha kuridhisha kwa benchi la ufundi la Madrid, hali inayozua maswali kuhusu mustakabali wake.
Inaelezwa kuwa uongozi wa Real Madrid haujamfunga Trent milango ya kutoka, na uko tayari kusikiliza ofa kutoka kwa klabu zitakazovutiwa na huduma yake. Baadhi ya mabosi wa klabu hiyo wanaamini kuwa mchezaji huyo hajaendana kikamilifu na falsafa ya timu, jambo linaloweza kuharakisha uamuzi wa kumuacha endapo ofa sahihi itawasilishwa.
Kwa upande wa Manchester City, nia ya kumsajili Trent inachangiwa na idadi kubwa ya majeruhi katika safu ya ulinzi, hali iliyomfanya kocha wao kuangalia chaguo mbadala lenye uzoefu wa juu katika soka la Ulaya.
Hadi sasa, Real Madrid bado haijatoa msimamo rasmi kuhusu mustakabali wa beki huyo wa zamani wa Liverpool, lakini dalili zinaonyesha kuwa milango ipo wazi kwa mazungumzo.Β