Mchezo wa nne kundi B ligi ya mabingwa barani Afrika kati ya Yanga dhidi ya Al Ahly umemalizika kwa matokeo ya sare ya bao 1-1.
Mchezo huo uliopigwa uwanja wa New Amaan Complex ulishuhudia Yanga ikitangulia kufunga dakika ya 45 kupitia Ibrahim Bacca baada ya piga nikupe langoni mwa Al Ahly kufuatia krosi ya Pacome Zouzoua kutoka upande wa kulia.

Yanga ilikuwa bora kwa muda mwingi wa mchezo hasa kipindi cha kwanza wakitengeneza nafasi nyingi kuliko wapinzani wao lakini hawakuweza kuzitumia.
Kipindi cha pili ni Al Ahly waliorejea na kasi kubwa wakisaka bao la kusawazisha huku Yanga wakiendelea kushambulia kwa kushitukiza.
Aliou Dieng ndiye aliyeisawazishia Al Ahly baada ya mpira wa kona ambao walinzi wa Yanga walizembea kuondoa.
Yanga ilipata nafasi adimu kwenye kipindi cha pili lakini Maxi Nzengeli hakuweza kuitumia huku Duke Abuya na Prince Dube wakipoteza nafasi pia.
Ni matokeo ambayo unaweza kusema yataziacha timu zote zikiridhika kwani ulikuwa mchezo ambao kila kitu ilitengeneza nafasi na pengine kushinda.
Yanga imefikisha alama tano ikiendelea kusalia nafasi ya pili kundi B huku Al Ahly wakiongoza na alama zao nane.