Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ali amewapa pole Wanasimba wote baada timu yao kushindwa kufuzu robo fainali ya ligi ya mabingwa leo wakilazimishwa sare ya mabao 2-2 dhidi ya Esperance.
Ahmed amesema ni msimu mbaya kwa Simba kushindwa kufuzu robo fainali baada ya kufanya hivyo kwa takribani misimu saba mfululizo.
Ahmed amesema kwa sasa Simba inaelekeza nguvu zake kwenye mechi mbili zilizobaki kukamilisha ratiba na kuwekeza nguvu kubwa zaidi kwenye mashindano ya ndani.
Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii, Ahmed ameandika ujumbe huu.
"Umekua msimu mbaya kwetu kwenye michuano ya kimataifa, inauma lakin hatuna budi kukubali kuwa msimu huu umekua mgumu kwetu
Kama ambavyo misimu mingine tunafuzu kwenda Robo Fainali na wengine wanashindwa basi msimu imekua zamu yetu kuanguka
Hatuna sababu ya kuvurugana wala kutafuta mchawi itoshe kusema msimu huu haukuwa wetu au haikua rizki yetu
Tumalizie mechi mbili zilizobaki baada ya hapo tuwekeze nguvu kwenye mashindano ya ndani huku bado tuna nafasi kubwa ya kufanya vizuri
Poleni ndugu zangu Wana Simba, Tulichozea kufanya tumeshindwa kufanya safari hii, Tukubali kuwa huu ni msimu mbaya kwetu na hutokea kwa timu yeyote Duniani
Asanteni na poleni wale wote waliotoa nguvu zao kuipambania Simba ishinde hii leo, Asanteni wale wote waliokuja Uwanjani hii leo, Tanatambua na kuthamini mchango wenu kwenye kuipambania Simba yetu
Itoshe kusema Asante Mungu wewe ndio mpangaji wa yote
Hadi wakati mwingine Wanyama, Hakuna kukataa tamaa maisha ya mpira bado yanaendelea"