Klabu ya AS FAR ya Morocco leo Jumamosi, Februari 7, itakuwa mwenyeji wa Young Africans (Yanga) ya Tanzania katika mchezo wa hatua ya makundi, Kundi B, wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) utakaopigwa kwenye Uwanja wa Olympic mjini Rabat.
Mchezo huo ni wa raundi ya tano ya makundi na unatarajiwa kuwa na ushindani mkali kutokana na umuhimu wake katika mbio za kusaka tiketi ya robo fainali.
Katika msimamo wa Kundi B, ushindani bado uko wazi huku timu zikipigania nafasi mbili za juu zitakazowezesha kufuzu hatua inayofuata. Yanga na AS FAR zinaingia katika mchezo huo zikiwa na pointi zinazozifanya ziwe kwenye presha ya kutafuta ushindi ili kujiweka katika mazingira mazuri kabla ya raundi ya mwisho.
Matokeo ya leo yanaweza kubadili kabisa mwelekeo wa kundi hilo. Ushindi kwa upande wowote utaiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu robo fainali, huku matokeo mengine yakiongeza presha kuelekea mchezo wa mwisho wa makundi.
Katika mchezo wa kwanza uliochezwa Tanzania, Yanga ilifanikiwa kuibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0, matokeo yanayoongeza mvuto wa pambano la leo. AS FAR watakuwa na hamu ya kulipa kisasi nyumbani mbele ya Yanga ambayo ina rekodi nzuri ya kufanya vizuri ugenini.
Ikumbukwe mchezo huo utachezwa bila mashabiki AS FAR wakitumikia adhabu ya CAF kufuatia vurugu za mashabiki wao kwenye mchezo dhidi ya Al Ahly.
Yanga, chini ya kocha Pedro Goncalves, wanaelewa wazi umuhimu wa mechi hiyo. Ushindi ugenini dhidi ya wapinzani wenye uzoefu kama AS FAR utakuwa hatua kubwa kuelekea robo fainali na uthibitisho wa uimara wao katika michuano hiyo.
Kwa upande wa AS FAR, timu hiyo imekuwa na rekodi nzuri wanapocheza nyumbani katika mashindano ya kimataifa, jambo linalofanya mchezo huo kutotabirika kutokana na ubora wa kila timu.
Kwa ujumla, pambano la leo linatajwa kuwa la maamuzi kwa timu zote mbili. Yanga wanahitaji ushindi au angalau sare ili kuendelea kuwa kwenye reli ya kufuzu, wakati AS FAR wakihitaji ushindi ili kujihakikishia nafasi nzuri kabla ya mchezo wa mwisho wa kundi.
Dua za mashabiki wa Yanga na Watanzania kwa ujumla ni kuwaombea wawakilishi hao wa nchi waibuke na ushindi ugenini na kama haitawezekana basi hata sare itafaa.
Ikumbukwe ni Yanga pekee yenye nafasi ya kuendelea kupeperusha bendera ya Tanzania hatua ya robo fainali kama itafanya vyema katika mchezo huo kwani watani zao Simba tayari wamepoteza matumaini ya kufuzu.



