Kocha Yanga anazitaka alama zote tatu Ruangwa

Joel JJ By Joel JJ β€’ 21st February 2026


Kocha Yanga anazitaka alama zote tatu Ruangwa

Kocha Mkuu wa Yanga Pedro Goncalves amesema kikosi chake kimejiandaa kikamilifu kuelekea mchezo wa ligi kuu dhidi ya Namungo Fc ambao utapigwa kesho Jumapili katika uwanja wa Majaliwa.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Goncalves amesema licha ya kukabiliwa na ratiba ngumu ya kucheza mechi mfululizo, wanakwenda kwenye mchezo huo wakiwa imara lengo likiwa kuchukua alama tatu.

Goncalves amewashukuru mashabiki wa timu hiyo waliojitokeza kwa wingi kuwapokea akiamini wameongeza hamasa kwa wachezaji wao.

"Kwanza kabisa napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa watu wote waliotupokea tangu tulipowasili. Mapokezi tuliyopata tangu tulipotua hadi kufika hapa yalikuwa mazuri sana na yametugusa kila mmoja wetu. Ninaamini kila mtu ana hamasa kubwa kuelekea mchezo wa kesho na nguvu hiyo tuliyopewa inatupa motisha kubwa"

"Kesho tutacheza dhidi ya Namungo FC, timu ambayo hadi sasa imekuwa na msimu mzuri sana. Nafikiri wako nafasi ya tano kwenye msimamo wa ligi. Ni timu imara sana wanapocheza nyumbani. Mara nyingi wamekuwa wakishinda mechi zao za nyumbani, jambo linaloonyesha ubora wao"

"Tunafahamu vizuri changamoto inayotusubiri kesho. Tunapitia ratiba yenye msongamano mkubwa wa mechi, lakini tunapaswa kucheza mechi moja baada ya nyingine. Kesho tutakuwa ugenini dhidi ya Namungo, lakini tutacheza kwa falsafa ileile tunayofuata katika kila mchezo. Mwisho wa siku tutafanya kila tuwezalo kupata alama tatu na kuendelea vizuri na safari yetu," alisema Goncalves

Aidha Goncalves amesema baadhi ya wachezaji watakosekana kutokana na changamoto za majeraha

"Kwa bahati mbaya tuna baadhi ya wachezaji wenye majeraha ambao hawakuweza kuja na timu. Aziz (Andambwile) alipata majeraha kidogo, bado tunaendelea kufuatilia hali yake lakini tuna matumaini si tatizo kubwa"

"Edmond pia ana majeraha aliyopata wiki iliyopita huenda akarejea mazoezini baada ya siku chache. Pacome alipata maumivu baada ya kugongana na kipa katika mchezo uliopita, hivyo hayuko katika hali nzuri kwa sasa."

"Kibwana na Mshery pia ni wagonjwa na hakuweza kusafiri. Dube alikuwa na tatizo la kiafya wakati wa mazoezi. Mzize anaendelea vizuri huku akipata uangalizi wa umakini kabla hajarejea tena kuwa nasi. Hata hivyo, wachezaji waliopo watafanya kila wawezalo kusaidia timu kupata alama tatu kesho," alisema


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.