Yanga S.C., Simba S.C., Azam F.C. na Singida Black Stars F.C. wameonyesha makali yao baada ya kurejea kutoka majukumu ya mashindano ya CAF kwa kushinda michezo yao ya viporo katika Ligi Kuu ya NBC.
Jana jumla ya mechi nne zilichezwa katika viwanja tofauti nchini, huku kila mmoja wa vigogo hao akikusanya pointi tatu muhimu.
Mapema mchana, Singida Black Stars walikuwa ugenini katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma, wakipambana na Mtibwa Sugar F.C.. Singida walionesha ubora mkubwa na kuibuka na ushindi wa mabao 3-1, matokeo yaliyowaongezea morali katika mbio za kusaka nafasi za juu.

Usiku majira ya saa 3:00, dimba hilohilo la Jamhuri lilishuhudia pambano kati ya Tanzania Prisons F.C. na Simba. Wekundu wa Msimbazi walitawala mchezo huo na kuibuka na ushindi wa mabao 2-0. Mabao ya Simba yalifungwa na Suleiman Mwalimu huku bao la pili likiwekwa wavuni na Rushine De Reuck kwa mkwaju wa penati.
Ushindi huo umeifanya Simba kufikisha alama 22 na kupanda hadi nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi, ikiendelea kujiweka katika mazingira mazuri ya kuwania nafasi za juu.

Katika Uwanja wa KMC Complex, KMC F.C. waliwakaribisha Azam FC. Hata hivyo, wenyeji waliendelea na mwendo wa kusuasua baada ya kukubali kipigo cha mabao 2-0. Mabao yote mawili ya Azam yalifungwa na mshambuliaji Idd Nado, aliyekuwa nyota wa mchezo huo.

Kwa upande mwingine, mabingwa watetezi Yanga walikuwa ugenini Ruangwa, mkoani Lindi, wakikabiliana na Namungo F.C.. Wananchi walipata ushindi mwembamba wa bao 1-0 lililofungwa na mshambuliaji Laurindo Aurélio ‘Depu’ kwa mkwaju wa penati. Ushindi huo umeifanya Yanga kufikisha alama 25 na kupanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.



