Klabu ya Arsenal imeendelea kuimarisha nafasi yake kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya England (EPL) baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Brighton katika mechi iliyochezwa Jumatano usiku.
Bao pekee la mchezo lilifungwa na Bukayo Saka, na kuisaidia Arsenal kujikusanyia pointi tatu muhimu katika mbio za ubingwa wa msimu huu. Ushindi huo umeifanya Arsenal kufikisha pointi 67 na kujiweka mbele kwa pointi saba dhidi ya Manchester City, ambao wana mchezo mmoja mkononi.
Katika mchezo mwingine uliovuta hisia nyingi, Manchester City walilazimishwa sare ya mabao 2-2 dhidi ya Nottingham Forest katika dimba la Etihad. City waliongoza mara mbili lakini Forest walifanikiwa kusawazisha kupitia Morgan Gibbs-White na Elliot Anderson na hivyo kuinyima City ushindi muhimu.
Wakati huo huo, Chelsea ilipata ushindi mkubwa wa mabao 4-1 dhidi ya Aston Villa ugenini katika uwanja wa Villa Park. Mshambuliaji João Pedro aliibuka shujaa wa mchezo huo baada ya kufunga mabao matatu (hat-trick), huku Cole Palmer naye akiongeza bao moja katika ushindi huo ulioiwezesha Chelsea kupanda hadi nafasi ya tano kwenye msimamo wa ligi.
Katika dimba la St James’ Park, Newcastle United iliifunga Manchester United mabao 2-1 licha ya kucheza kipindi cha pili ikiwa na wachezaji 10 uwanjani baada ya Jacob Ramsey kutolewa kwa kadi nyekundu. Bao la ushindi lilifungwa dakika za mwisho na William Osula na hivyo kumaliza rekodi ya Manchester United ya kutopoteza mechi chini ya kocha wa muda Michael Carrick.
Katika mchezo mwingine wa usiku huo, West Ham United iliibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Fulham, ushindi uliowasaidia kujinasua kidogo katika vita vya kuepuka kushuka daraja.
Matokeo Kamili ya Mechi (Machi 4, 2026)
Aston Villa 1 – 4 Chelsea
Brighton 0 – 1 Arsenal
Fulham 0 – 1 West Ham United
Manchester City 2 – 2 Nottingham Forest
Newcastle United 2 – 1 Manchester United
Kwa matokeo hayo, mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya England zimeendelea kupamba moto huku Arsenal ikionekana kuwa na nafasi nzuri ya kutwaa taji, wakati ushindani wa nafasi za juu pamoja na vita vya kushuka daraja ukiendelea kuwa mkali kadri msimu unavyoelekea ukingoni.



