Beki wa Simba Rushine de Reuck amesema mapokezi mazuri na sapoti anayopata kutoka kwa Wanasimba ni moja ya sababu iliyopelekea akubali kuendelea kuitumikia Simba kwa muda mrefu zaidi.
Rushine jana alisaini mkataba wa mwaka mmoja kuendelea kuitumikia Simba ambao utamfanya asalie Msimbazi hadi mwishoni mwa msimu wa 2027.
"Nimefurahi sana kuongeza mkataba kuendelea kusalia hapa. Tangu siku nilipojiunga na Simba, nimekuwa na uhusiano wa kipekee na mashabiki wa Simba."
"Wamenipokea vizuri na pia wananipa ushirikiano hivyo uamuzi huu wa kuongeza mkataba ni kama kurudisha shukrani kwao," alisema Rushine.
Rushine ambaye amekabidhiwa majukumu ya unahodha msaidizi wa Simba, amekuwa na wakati mzuri tangu alipojiunga na Simba kwenye usajili uliopita wa dirisha kubwa akitokea klabu ya Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini.
Wakati anatua alisaini mkataba wa mkopo wa mwaka mmoja ambao ulikuwa na kipengele cha kuongeza mwaka wa pili.
Beki huyo alikuwa akiwaniwa kwa karibuni na Raja CA inayonolewa na kocha Fadlu Davids ambaye alichangia kwa kiasi kikubwa kumleta Simba wakati anawanoa Wekundu hao wa Msimbazi.
Simba pia imemuongeza mkataba kiungo wake mkabaji Yusuph Kagoma ambaye ameongeza mkataba wa miaka miwili ambao utamuweka Msimbazi hadi mwaka 2028.
>>> XTRA 90 MEDIA imetangaza nafasi za kazi. BONYEZA HAPA



