Kocha Mkuu wa Simba Steve Barker amesema kikosi chake kimejiandaa kushinda mchezo wa ligi kuu dhidi ya Singida Black Stars ambao utapigwa kesho Jumatano katika uwanja wa Airtel huko Singida.
Akizungumza katika mkutano na wanahabari mapema leo kuelekea mchezo huo, Barker alisema hawakushinda mechi mbili zilizopita kwenye ligi hiyo mchezo huo una umuhimu wa kipekee kwao kushinda.
"Ni mchezo muhimu sana kwetu, hatukushinda michezo miwili liyopita, hivyo huu ni mchezo muhimu kwetu kushinda ili kurejea kwenye nafasi nzuri katika mbio za ubingwa."
"Tunatambua Singida BS ni timu nzuri wamekuwa na msimu bora mpaka sasa pia wana kocha mzuri hivyo lazima tuhakikishe kesho tunacheza katika ubora wetu ili tuwe na nafasi nzuri ya kushinda."
"Tunawaahidi mashabiki wetu tutajiandaa vyema na kucheza katika mpango sahihi wa mchezo ili tuhakikishe tunawapa furaha," alisema Barker
Nae kocha msaidizi wa Singida Black Stars David Ouma, amesema wamejiandaa kutumia vyema uwanja wa nyumbani na kuondoka na ushindi katika mchezo huo.

Ouma amesema malengo ya Singida BS msimu huu ni kutwaa ubingwa hivyo wanapaswa kushinda mechi kubwa ili kufikia matarajio yao.
"Sisi Singida tunajiona kama moja ya timu zinazowania ubingwa wa ligi kuu. Ili uwe bingwa unapaswa kushinda mechi kubwa kama hii dhidi ya Simba. Hivyo tumejipanga kuhakikisha tunaibuka na ushindi," alisema Ouma