Mbeya City wapigwa 4G na Singida BS

Joel JJ By Joel JJ • 15th March 2026


Mbeya City wapigwa 4G na Singida BS

Timu ya Singida Black Stars F.C. imepata ushindi mnono wa mabao 4-1 dhidi ya Mbeya City F.C.< katika mchezo wa NBC Premier League uliochezwa Jumapili, Machi 15, 2026, majira ya saa 10 jioni katika Uwanja wa Tanzanite Kwaraa Stadium uliopo Babati, mkoani Manyara.

Katika mchezo huo wa ligi kuu Tanzania Bara, Singida Black Stars walionyesha kiwango kizuri hasa katika kipindi cha pili na kufanikiwa kuondoka na pointi tatu muhimu.

Mchezo ulianza kwa kasi huku Mbeya City wakionyesha nia ya kusaka ushindi mapema. Dakika ya 14, mshambuliaji Vitalis Mayanga aliifungia Mbeya City bao la kuongoza na kuwapa matumaini mashabiki wao.

Hata hivyo, furaha hiyo haikudumu kwa muda mrefu baada ya Singida Black Stars kusawazisha matokeo kupitia kwa Emmanuel Keyekeh aliyefunga kwa mkwaju wa penalti katika dakika ya 32 na kufanya matokeo kuwa 1-1 kabla ya mapumziko.

Kipindi cha pili kilishuhudia Singida Black Stars wakiongeza kasi ya mashambulizi na kuanza kutawala mchezo.

Dakika ya 70, Mossi Nduwumwe aliifungia Singida bao la pili na kuifanya timu yake kuanza kuongoza mchezo. Dakika nne baadaye, kiungo Ibrahim Imoro alifunga bao la tatu na kuongeza presha kwa Mbeya City.

Imoro alirudi tena kambani katika dakika ya 88, akifunga bao lake la pili binafsi na la nne kwa Singida Black Stars, bao lililohitimisha ushindi huo wa mabao 4-1.

Ushindi huo ni muhimu kwa Singida Black Stars katika mbio za kujipanga kwenye msimamo wa ligi, huku Mbeya City wakiendelea kutafuta matokeo bora katika mechi zao zijazo. 


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.