Mshambuliaji wa Simba, Jonathan Sowah, amejitetea rasmi mbele ya kamati ya nidhamu ya klabu kufuatia kusimamishwa kwake kutokana na tuhuma mbalimbali za utovu wa nidhamu. Uongozi wa Simba ulimpa nafasi ya kusikilizwa ili kutoa maelezo yake kabla ya maamuzi ya mwisho kuhusu hatma yake ndani ya klabu hiyo.
Katika utetezi wake, Sowah amekanusha baadhi ya tuhuma zilizotolewa dhidi yake huku akikiri makosa madogo aliyoyafanya, akisisitiza kuwa bado ana nia na dhamira ya kuitumikia Simba.
Akanusha Kukataa Mazoezi
Akijibu tuhuma kwamba alikataa kufanya mazoezi Februari 17 katika maandalizi ya mchezo dhidi ya Greenland FC, Sowah amesema madai hayo si ya kweli. Ameeleza kuwa alishiriki kikamilifu kwenye activation session licha ya kuwa tayari alikuwa amesimamishwa, hali iliyomzuia kushiriki mazoezi kamili au kucheza uwanjani.
Amesema baada ya kumaliza mazoezi hayo mafupi, kocha wa viungo alimruhusu kuondoka, jambo ambalo linaonyesha kuwa hakukataa kushiriki mazoezi kama ilivyodaiwa.
Mazoezi ya Ziada (Top-up Training)
Kuhusu mazoezi ya ziada yaliyotajwa kufanyika Februari 22, Sowah amesema kulikuwa na mkanganyiko uliotokana na changamoto za kiutendaji ikiwemo basi la timu kuchelewa pamoja na kukosekana kwa vifaa vyake vya mazoezi.
Amefafanua kuwa mazoezi hayo yalifanyika baadaye hotelini pamoja na wachezaji wenzake chini ya usimamizi wa kocha wa viungo. Aidha, amesema kuna ushahidi wa video unaoweza kuthibitisha kuwa alishiriki kikamilifu kwenye mazoezi hayo.
Akiri Kuchelewa Mazoezini
Sowah pia amekiri kuchelewa kwa takribani dakika tano kwenye mazoezi ya Februari 16. Ameeleza kuwa kuchelewa huko kulitokana na kusinzia bila kukusudia baada ya kikao kirefu cha uchambuzi wa video.
Kwa mujibu wake, mara tu alipogundua amechelewa alimjulisha kocha na kusisitiza kuwa haikuwa kwa makusudi.
Akataa Kuchelewa Vikao vya Timu
Katika hoja nyingine, mshambuliaji huyo amekanusha vikali madai kwamba amewahi kuchelewa kwenye vikao vya timu. Amesema amekuwa akiheshimu ratiba zote za vikao tangu ajiunge na klabu hiyo.
Tuhuma za Kuvaa Jezi Isiyo Rasmi
Kuhusu madai kwamba alivaa jezi ya Benfica wakati wa safari ya timu kwenda Angola, Sowah amesema hilo si kweli. Ameeleza kuwa alivaa jezi rasmi ya Simba SC na kuongeza kuwa ushahidi unaweza kupatikana kupitia picha zilizochapishwa kwenye mitandao rasmi ya klabu.
Tuhuma za Faulo “Zisizo za Kawaida”
Akijibu hoja kuhusu kufanya faulo zisizo za kawaida uwanjani, Sowah amesema vitendo hivyo vilikuwa sehemu ya ushindani wa kawaida wa mpira wa miguu. Amesisitiza kuwa hakuwahi kuwa na nia ya makusudi kumdhuru mpinzani au kutafuta kadi nyekundu.
Akanusha Tetesi za Rushwa
Kwa upande wa tetesi za kupokea fedha kutoka klabu za Young Africans SC au Singida Black Stars, Sowah amekanusha vikali madai hayo akiyataja kuwa ni ya uongo na yanayoharibu sifa yake kama mchezaji wa kulipwa.
Ameiomba Simba kuchunguza kwa kina tuhuma hizo na kutoa ufafanuzi hadharani ili kulinda heshima yake.
Ombi Lake kwa Klabu
Sowah amesema bado ana nia ya dhati ya kuitumikia Simba na kusaidia timu kufikia malengo yake. Ameuomba uongozi wa klabu hiyo uondoe adhabu ya kusimamishwa au uharakishe mchakato wa kinidhamu ili aweze kurejea uwanjani na kuendelea na kazi yake ya soka.
Kwa sasa, kinachosubiriwa ni uamuzi wa kamati ya nidhamu ya Simba kuhusu hatma ya mshambuliaji huyo.



