Nahodha wa Manchester United, Bruno Fernandes, ameandika historia mpya katika klabu hiyo baada ya kuvunja rekodi iliyodumu kwa zaidi ya miaka 25 iliyowekwa na gwiji wa zamani David Beckham.
Rekodi hiyo ilivunjwa katika mchezo wa Ligi Kuu England ambapo Manchester United iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Aston Villa kwenye uwanja wa Old Trafford. Katika mechi hiyo, Fernandes alitoa pasi mbili za mabao (assists) zilizosaidia timu yake kupata ushindi muhimu.
Kwa pasi hizo mbili, kiungo huyo wa kimataifa wa Ureno alifikisha assist 16 katika msimu wa 2025/26 wa Ligi Kuu England, hivyo kuvunja rekodi ya assists 15 ambayo Beckham aliweka katika msimu wa 1999/2000 akiwa Manchester United.
Mbali na kuvunja rekodi hiyo ya kihistoria, Fernandes pia alifikisha assist ya 100 akiwa na Manchester United katika mashindano yote, jambo linalothibitisha mchango wake mkubwa kwa timu tangu alipojiunga mwaka 2020.
Katika mchezo huo, mabao ya Manchester United yalifungwa na Casemiro, Matheus Cunha, na Benjamin Sesko, huku Villa wakipata bao lao kupitia Ross Barkley. Ushindi huo uliisaidia United kuimarisha nafasi yao katika mbio za kufuzu michuano ya Ulaya msimu ujao.
Baada ya kuvunja rekodi hiyo, Fernandes alisema ni heshima kubwa kuvuka rekodi ya Beckham, ambaye ni mmoja wa wachezaji waliowahi kuipa Manchester United mafanikio makubwa. Aliongeza kuwa rekodi hiyo haitabadilisha malengo yake ya kuendelea kusaidia timu kushinda mataji.
Kwa sasa, Fernandes anaendelea kuwa moja ya wachezaji muhimu zaidi katika kikosi cha Manchester United na anatajwa miongoni mwa wanaowania tuzo ya Mchezaji Bora wa Ligi Kuu England msimu huu kutokana na kiwango chake bora.