Klabu kubwa barani Ulaya zinaendelea kupiga hesabu za kujiimarisha kuelekea dirisha lijalo la usajili, huku tetesi mbalimbali zikihusisha nyota kadhaa wakubwa wa soka.
Taarifa kutoka England zinaeleza kuwa FC Barcelona wanapanga kujaribu kumbakisha mshambuliaji wa Manchester United, Marcus Rashford, kwa mkopo kwa msimu mwingine. Hatua hiyo inalenga kuepuka kulipa ada ya uhamisho inayokadiriwa kufikia pauni milioni 26.
Wakati huo huo, Manchester United wanatajwa kuangalia uwezekano wa kumsajili kiungo wa Nigeria Wilfred Ndidi kutoka Beikta JK. Inaelezwa kuwa dili hilo linaweza kuhusisha kubadilishana na kipa wa Uturuki Altay Bayndr, ambaye huenda akaelekea upande wa klabu hiyo ya Istanbul.
Nchini Ujerumani, Borussia Dortmund wanaamini wana nafasi kubwa ya kumshawishi winga wa Manchester United, Jadon Sancho, kurejea katika klabu hiyo kwa mara ya tatu.
Aidha, United wanaendelea kuonyesha nia ya kumsajili kiungo wa Italia Sandro Tonali kutoka Newcastle United. Hata hivyo, Newcastle wanadaiwa kuweka bei ya zaidi ya pauni milioni 100 kwa mchezaji huyo.
Kwa upande wa Italia, Juventus FC wamepewa nafasi ya kumsajili mshambuliaji wa Uholanzi Joshua Zirkzee kutoka Manchester United kwa euro milioni 25, ingawa pia wanatazamia mpango wa mkopo wenye kipengele cha kumnunua baadaye.
Katika harakati nyingine, Newcastle wanamfuatilia kiungo wa Senegal Lamine Camara, ambaye anaweza kuondoka AS Monaco majira ya kiangazi. Klabu hiyo pia inatajwa kumtaka kipa chipukizi wa Ufaransa Robin Risser kutoka RC Lens.
Nayo West Ham United inapanga kufanya mazungumzo na Chelsea FC ili kubadilisha mkopo wa beki wa Ufaransa Axel Disasi kuwa uhamisho wa kudumu.
Katika hatua nyingine, Chelsea pamoja na Tottenham Hotspur wanatajwa kumuwania mshambuliaji wa TSG Hoffenheim, Fisnik Asllani.



