Rais wa CAF Patrice Motsepe, amevunja ukimya kufuatia uamuzi tata wa kuinyang’anya Senegal ubingwa wa Mataifa ya Afrika 2025 (AFCON) na kuipatia Morocco, akisisitiza kuwa maamuzi ya vyombo vya kisheria vya shirikisho hilo yanapaswa kuheshimiwa.
Motsepe alieleza kuwa uamuzi huo ulitolewa na kamati huru ya rufaa ya CAF kwa kuzingatia kanuni za mashindano, na hivyo haukuwa wa kisiasa bali wa kisheria. Amesisitiza kuwa CAF ina wajibu wa kusimamia sheria na kuhakikisha haki inatendeka kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.
Uamuzi huo ulitangazwa rasmi Machi 17, 2026, baada ya kamati ya rufaa kubaini kuwa timu ya Senegal ilikiuka kanuni kwa kuondoka uwanjani bila ruhusa ya mwamuzi wakati wa fainali dhidi ya Morocco. Kwa mujibu wa kanuni hizo, kitendo hicho kinachukuliwa kama kupoteza mechi, na hivyo matokeo kubadilishwa kuwa ushindi wa mabao 3-0 kwa Morocco.
Awali, Senegal walikuwa wameshinda mchezo huo kwa mabao 1-0 baada ya muda wa nyongeza, lakini mechi hiyo iligubikwa na utata mkubwa kufuatia wachezaji wao kutoka nje ya uwanja wakipinga penalti iliyotolewa kwa Morocco dakika za mwisho.
Hata hivyo, kauli ya Motsepe imekuja wakati kukiwa na upinzani mkubwa kutoka Senegal, ambapo serikali na shirikisho la soka la nchi hiyo zimeutaja uamuzi huo kuwa si wa haki na zimetangaza kupeleka rufaa katika Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS).
Sakata hilo limeibua mjadala mpana barani Afrika na duniani, huku baadhi ya wadau wa soka wakikosoa uamuzi huo na wengine wakisisitiza umuhimu wa kufuata sheria za mchezo.
Licha ya presha hiyo, Motsepe amesisitiza kuwa CAF itaendelea kulinda misingi ya haki, uwazi na utawala bora katika soka la Afrika.



