Wekundu wa Msimbazi, Simba Sc wameshindwa kunufaika na matokeo ya watani zao Yanga baada ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Pamba Jiji katika mchezo wa ligi kuu uliopigwa uwanja wa CCM Kirumba.
Jana Yanga ililazimishwa suluhu ya bila kufungana dhidi ya TRA United na kuibua shangwe kwa mashabiki wa Simba wakiamini wana nafasi ya kupunguza gap la pointi dhidi ya watani zao hao kwenye msimamo wa ligi.
Anicet Oura aliitanguliza Simba kwa bao safi kwenye dakika ya 33 lakini Pamba Jiji wakarejea mchezoni dakika tatu baadae James Mwashinga akifunga bao kwa shuti kali lililomshinda mlinda lango wa Simba Djibril Kassali kupitia mpira wa adhabu.
Licha ya kutawala mchezo huo, Simba walishindwa kuipenya ngome ya Pamba Jiji na kupelekea mchezo huo kumalizika kwa matokeo ya sare.
Mchezo mwingine wa ligi kati ya Mashujaa Fc dhidi ya Azam Fc ulipigwa uwanja wa Lake Tanganyika mkoani Kigoma na kumalizika kwa matokeo ya suluhu ya bila kufungana.
Matokeo hayo yamepelekea kutokuwa na mabadiliko makubwa kwenye msimamo wa ligi, Azam Fc wakiendelea kusalia nafasi ya pili huku Simba wakisogea nafasi ya tatu.



