Kocha Mkuu wa Yanga Pedro Goncalves amesisitiza kuwa kikosi chake hakipati muda wa kutosha wa maandalizi ya mechi kutokana na ratiba ngumu inayaowakabili.
Yanga iko mkoani Dodoma ambapo kesho Jumamosi, watashuka uwanja wa Jamhuri kuikabili Mtibwa Sugar katika mchezo wa mzunguuko wa 16 ambao ni wa kwanza duru ya pili.
Akizungumza na wanahabari mapema leo kuelekea mchezo huo, Goncalves alisema kesho watacheza mechi ya 7 katika kipindi cha siku 21.
Amesema kwa takribani wiki tatu wanacheza ugenini katika mechi ambazo zinawalazimu kusafiri huku baadhi ya wachezaji wakiwa kwenye mfungo.
Hata hivyo kocha huyo raia wa Ureno amesisitiza kuwa pamoja na changamoto hizo, wataendelea kupambana wakijipanga kupata ushindi kwenye mchezo dhidi ya Mtibwa Sugar.
"Maandalizi yetu kuelekea mchezo wa kesho yamekuwa na changamoto kubwa. Tulitoka Arusha jana baada ya safari ndefu na tulipowasili hapa, wachezaji wengi walifanya mazoezi ya kurejesha nguvu (recovery), huku wengine wakifanya mazoezi mepesi uwanjani."
"Kwa kipindi cha wiki tatu hadi nne zilizopita tumekuwa na ratiba ngumu sana. Mchezo wa kesho utakuwa wa saba ndani ya siku 21 jambo ambalo ni changamoto kubwa. Pia tunapaswa kuzingatia kuwa baadhi ya wachezaji wako kwenye mfungo wa Ramadhani pamoja na safari za mara kwa mara kwa ujumla tunapitia kipindi kigumu sana cha msimu"
"Tumemaliza mzunguko wa kwanza wa ligi tukiwa kileleni mwa msimamo. Hili halitupi ubingwa, lakini linatupa imani kubwa kuelekea siku zijazo. Sasa tunaelekeza nguvu zetu kwenye mchezo wa kesho dhidi ya Mtibwa Sugar."
"Kwangu binafsi, huu ni mchezo wa kipekee. Ulikuwa mchezo wangu wa kwanza nikiwa na timu hii nyumbani uliochezwa KMC. Wakati huo hatukuwa kileleni tulikuwa nyuma kwa alama mbili dhidi ya wapinzani wetu. Sasa tupo juu ya msimamo tunapoanza mzunguko wa pili na kujiamini kutakuwa muhimu sana"
"Lengo letu siku zote ni pointi tatu na kesho haitakuwa tofauti. Pia ni muhimu kwetu kufika kwenye dirisha la mechi za kimataifa (FIFA) tukiwa kileleni bila kujali matokeo ya kesho. Kipindi hicho kitakuwa muhimu kwa mapumziko na kurejea kwa wachezaji, hasa kwa wale walio na majeraha na watakaojiunga na timu zao za taifa," alisema Goncalves



