Mnyama Simba Sc ametakata uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo leo akiibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya TRA United katika mchezo wa ligi kuu ya NBC.
Unaweza kusema TRA United leo walikutana na soka la aina tofauti kabisa kutoka kwa vijana wa kocha Steve Barker waliokuwa na kiu ya alama tatu.
Simba iliandika bao la kwanza mapema tu kwenye dakika ya 12 kupitia kwa Suleiman Mwalimu aliyefunga bao lake la tano msimu huu.
Ulikuwa mkwaju wa penati baada ya Nickson Kibabage kufanyiwa madhambi katika eneo la hatari.
Simba ilikwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0, uongozi ambao uliwaongezea ari zaidi waliporejea kipindi cha pili.
Kasi ya Simba kupitia washambuliaji wa pembeni Libasse Gueye na Annicet Oura iliwapa wakati mgumu walinzi wa TRA United wakijikuta wanafanya madhambi mara kwa mara.
Kupitia mpira wa adhabu Neo Maema akaongeza bao la pili dakika ya 67 kabla ya Yusuph Kagoma kuongeza bao la tatu wakati mchezo ukielekea ukiongoni.
Ulikuwa mchezo ambao pengine Simba ingefunga mabao zaidi kama washambuliaji wake wangekuwa makini Elie Mpanzu akikosa miongoni mwa nafasi ya adimu dakika za lala salama.
Ni alama tatu muhimu kwa Simba ambazo zinawapaisha hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wakifikisha alama 31 na kuipiku Azam Fc yenye alama 29.
Simba bado ina mechi mbili za viporo dhidi ya vinara wa ligi hiyo Yanga wenye alama 38 baada ya mechi 16.



