Klabu ya Al Ittihad SC Tripoli ya Libya imeanza rasmi enzi mpya chini ya kocha wake mkuu, Rulani Mokwena, baada ya kuwasili mjini Fes kwa ajili ya kambi ya mazoezi ya siku 10.
Hatua hiyo inakuja ikiwa ni wiki moja tu tangu kocha huyo raia wa Afrika Kusini atangazwe rasmi kuinoa timu hiyo mnamo Machi 17, 2026, akitokea klabu ya MC Alger ya Algeria.
Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya klabu, kambi hiyo inalenga kujiandaa na mwendelezo wa Ligi Kuu ya Libya pamoja na kumpa nafasi kocha huyo kuwafahamu wachezaji wake na kuanza kutekeleza mbinu zake za kiufundi.
Mokwena, anayejulikana kwa falsafa yake ya soka la pasi nyingi na kasi maarufu kama “Rhulani-ball”, anatarajiwa kutumia muda huo kuimarisha mshikamano wa kikosi na kuweka msingi wa mfumo wake wa uchezaji.
Katika hatua inayoongeza matarajio kwa mashabiki, kocha huyo ameungana tena na baadhi ya wachezaji aliowahi kufanya nao kazi, akiwemo Thembinkosi Lorch pamoja na kiungo mshambuliaji Stephane Aziz Ki, ambaye aliwahi kung’ara katika klabu ya Young Africans SC.
Kwa sasa, Al Ittihad SC Tripoli ipo nyuma ya mahasimu wao wakubwa, Al Ahly Tripoli, kwa tofauti ya pointi sita katika msimamo wa ligi. Hata hivyo, wana michezo miwili mkononi ambayo inaweza kubadilisha mwelekeo wa mbio za ubingwa.
Mashabiki wa klabu hiyo wamepokea kwa shauku ujio wa Mokwena, wakiamini uzoefu wake katika soka la Afrika unaweza kuirejesha timu hiyo kwenye ubora wake wa zamani.



