Hawa Spurs Championship inawaita

Joel JJ By Joel JJ β€’ 25th March 2026


Hawa Spurs Championship inawaita

Klabu ya Tottenham Hotspur imeingia katika hofu kubwa ya kushuka daraja kufuatia kipigo kizito cha mabao 3-0 kutoka kwa Nottingham Forest mwishoni mwa wiki iliyopita katika mchezo wa Ligi Kuu England.

Katika pambano hilo muhimu kwa pande zote mbili zilizokuwa zikisaka pointi za kujinasua kutoka mkiani, Forest walionyesha ubora mkubwa kwa kufunga mabao kupitia Morgan Gibbs-White,Taiwo Awoniyi pamoja na Igor Jesus, na kuondoka na ushindi mnono uliowaacha Spurs hoi.

Matokeo hayo yameifanya Tottenham kushuka hadi nafasi ya 17 katika msimamo wa ligi, wakibaki juu ya mstari wa kushuka daraja kwa tofauti alama moj tu dhidi ya West Ham. Spurs wana alama 30 huku West Ham wakiwa na alama 29. Hali hiyo imezidisha presha kwa kikosi hicho ambacho kimekuwa kikisuasua kwa muda mrefu sasa.

Tottenham wanakabiliwa na rekodi mbaya ya kutopata ushindi katika mechi kadhaa mfululizo za ligi, jambo linaloonyesha wazi kuporomoka kwa kiwango cha timu hiyo. Ulinzi wao umekuwa dhaifu, huku safu ya ushambuliaji ikishindwa kutumia nafasi wanazozipata.

Kwa upande mwingine, ushindi huo umeipa Nottingham Forest nguvu mpya katika harakati zao za kubaki ligi kuu, wakipanda juu ya Tottenham katika msimamo baada ya kufikisha alama 32.

Kocha wa Tottenham, Igor Tudor, sasa anakabiliwa na shinikizo kubwa kutoka kwa mashabiki na uongozi wa klabu hiyo, huku wengi wakitaka mabadiliko ya haraka ili kuinusuru timu isishuke daraja.

Mashabiki wa Spurs walionyesha kutoridhishwa kwao wakati wa mchezo huo, baadhi wakiondoka uwanjani kabla ya kipenga cha mwisho, ishara ya kuchoshwa na matokeo mabaya yanayoendelea.

Huku msimu ukiwa unaelekea ukingoni, Tottenham sasa wanakabiliwa na mechi chache zilizosalia ambazo zinaweza kuamua hatima yao. Wataalamu wa soka wanaamini kuwa bila mabadiliko ya haraka ya mbinu na morali ya wachezaji, klabu hiyo inaweza kujikuta ikishuka daraja kwa mara ya kwanza katika kipindi kirefu.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.