Wito wa kumrejesha mshambuliaji nyota Neymar katika kikosi cha timu ya taifa ya Brazil kuelekea Kombe la Dunia 2026 umeendelea kushika kasi, huku kocha mkuu Carlo Ancelotti akisisitiza kuwa hatayumbishwa na shinikizo la mitandao ya kijamii katika maamuzi yake ya uteuzi.
Baadhi ya wachezaji wa Brazil, akiwemo Vini Jr, wametaja wazi kuwa uwepo wa Neymar ni muhimu kwa mafanikio ya timu hiyo, wakiamini uzoefu na ubora wake vinaweza kuisaidia Brazil katika mashindano yajayo.
Neymar, ambaye ni mfungaji bora wa muda wote wa Brazil akiwa na mabao 79, bado ana matumaini ya kushiriki Kombe la Dunia 2026 licha ya kukumbwa na majeraha yanayomuweka nje ya uwanja mara kwa mara tangu mwaka 2023.
Hata hivyo, kocha Ancelotti hajamjumuisha Neymar katika vikosi vya hivi karibuni vya maandalizi, hatua iliyozua mjadala mkubwa miongoni mwa mashabiki na wadau wa soka nchini humo.
Akizungumzia suala hilo, Ancelotti alieleza kuwa uteuzi wa kikosi unategemea vigezo vya kitaalamu, ikiwemo kiwango cha mchezaji, utimamu wa mwili na mchango wa kikosi, na si presha ya nje au mitandao ya kijamii.
“Maamuzi ya kikosi hayatategemea mitandao ya kijamii au maoni ya watu, bali kile ambacho ni bora kwa timu,” alisema Ancelotti.
Kauli hiyo inakuja wakati Neymar mwenyewe akitajwa kuonyesha hisia zake kupitia mitandao ya kijamii kufuatia kutokuitwa kwake, jambo lililochochea mjadala mkubwa zaidi.
Pamoja na hali hiyo, bado kuna uwezekano wa Neymar kurejea kikosini iwapo ataendelea kuimarika kimwili na kuonyesha kiwango bora katika klabu yake ya Santos.
Hata hivyo, muda unaonekana kuwa finyu, huku kikosi cha mwisho cha Brazil kwa Kombe la Dunia kikitarajiwa kutangazwa wiki chache zijzo.



