Kocha Mkuu wa Young Africans SC, Pedro Goncalves, unaweza kusema kwa kuangalia takwimu 'hajafeli' lakini kinachofanya ahukumiwe ni pale timu yake inaposhindanishwa na Yanga ya msimu uliopita.
Pedro alitambulishwa rasmi Oktoba 25, 2025 siku ambayo Yanga SC ilikuwa dimbani ikicheza dhidi ya Silver Strikers katika hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, huku yeye akifuatilia mchezo huo kwa njia ya televisheni.
Kocha huyo alianza rasmi majukumu yake kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mtibwa Sugar katika mchezo wa Ligi Kuu, ushindi ulioweka msingi wa mwenendo mzuri kwenye ligi.
Katika kipindi chake hadi sasa, Pedro ameiongoza Yanga katika jumla ya michezo 26 kwenye michuano minne tofauti ambayo ni Ligi Kuu, Ligi ya Mabingwa Afrika, Kombe la Shirikisho la CRDB na Kombe la Mapinduzi.
Kwa mujibu wa takwimu, kati ya michezo hiyo 26:
- Amefanikiwa kushinda michezo 17
- Sare 7
- Kupoteza mara 2 pekee
Aidha, timu imefunga jumla ya mabao 48 huku ikiruhusu mabao 8 tu, ikiashiria uimara mkubwa wa safu ya ulinzi pamoja na ufanisi wa ushambuliaji.
Katika Ligi Kuu pekee, Pedro ameiongoza Yanga kushinda michezo 10 kati ya 14 na kutoka sare mechi 4. Katika Ligi ya Mabingwa Afrika, timu imeshinda mechi 2, sare 2 na kupoteza 2.
Kwa upande wa Kombe la Mapinduzi, Yanga iliibuka mabingwa ikishinda mechi 3 na kutoka sare 1, huku kwenye Kombe la Shirikisho la CRDB ikishinda michezo yote miwili iliyocheza.
Sare tatu mfululizo katika mechi za ligi kuu ndio matokeo yaliyoweka rehani kibarua chake kabla ya uongozi wa Yanga kuridhia aendelee na majukumu yake baada ya tathmini huku wakimuongezea nguvu kwa kumrejesha Kocha Msaidizi Abduhamid Moalin.
Bado kikosi chake kiko kileleni mwa msimamo wa ligi huku akiahidia kurejesha ubingwa wa ligi Jangwani kwa msimu wa tano mfululizo



