Jumatano April 1 2026 Singida Black Stars wataikaribisha Azam Fc katika mchezo wa ligi kuu ya NBC utakaopigwa uwanja wa Airtel, mkoani Singida.
Baada ya kupoteza mechi mbili kubwa dhidi ya Yanga (3-0) na Simba (2-1) katika uwanja wake wa nyumbani, Singida BS inahitaji kujisahihisha dhidi ya 'mkubwa' mwingine kutoka jijini Dar es salaam.
Ukiacha mechi hizo walizopoteza dhidi ya 'wakubwa' hao kutoka Kariakoo, Singida BS imekuwa na mwenendo mzuri katika mechi zilizopita ikiibuka na ushindi.
Katika mechi tano zilizopita, Singida BS wamepoteza mechi mbili pekee dhidi ya Yanga na Simba na kushinda tatu.
Kwenye msimamo wa ligi wanashika nafasi ya sita wakiwa na alama 25 ambapo ushindi dhidi ya Azam Fc unaweza kuwasogeza hadi nafasi ya nne.
Kwa upande wa Azam Fc inayonolewa na kocha Florent Ibenge, ni timu ngumu kufungika msimu huu licha ya kuwa imedondosha alama nyingi kupitia matokeo ya sare.
Azam Fc haijapoteza mchezo wowote katika mechi 15 walizocheza duru ya kwanza. Lakini katika mechi tano zilizopita, imeshinda mechi moja tu na kutoka sare nyingine nne. Inashikilia nafasi ya tatu ikiwa imekusanya alama 29 baada ya kushuka dimbani mara 15.Β
Mchezo wa duru ya kwanza uliopigwa uwanja wa Azam Complex, ulimalizika kwa timu hizo kugawana pointi baada ya kutoka suluhu ya bila kufungana.
Je Singida BS wataweza kutumia vyema uwanja wao wa nyumbani siku ya Jumatano?