Stars yaifumua Macau 6-0 FIFA Series

Joel JJ By Joel JJ • 29th March 2026


Stars yaifumua Macau 6-0 FIFA Series

Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, imeibuka na ushindi mkubwa wa mabao 6-0 dhidi ya Macau katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki wa mashindano ya FIFA Series uliochezwa leo Jumapili kwenye Uwanja wa Pelé, Kigali nchini Rwanda.

Taifa Stars ilianza mchezo huo kwa kasi na kufungua ukurasa wa mabao dakika ya 16 kufuatia bao la kujifunga la mchezaji wa Macau, hali iliyowapa Tanzania kujiamini mapema. Shinikizo liliendelea kwa upande wa Tanzania na dakika ya 26 beki Bakari Mwamnyeto alifunga bao la pili kwa kichwa.

Kiungo Mudathir Yahya aliendeleza ubabe huo dakika ya 45 kwa kufunga bao la tatu, na kuiwezesha Tanzania kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 3-0.

Kipindi cha pili kiliendelea kuwa cha upande mmoja, huku Tanzania ikiendeleza mashambulizi makali dhidi ya wapinzani wao. Dakika ya 56, mshambuliaji Paul Peter alifunga bao la nne kabla ya Novatus Miroshi kuongeza la tano dakika ya 74.

Bao la sita na la mwisho lilifungwa dakika ya 87 na Tarryn Allarakhia, akiweka muhuri wa ushindi mnono kwa Taifa Stars.

Katika mchezo huo, Tanzania ilionyesha ubora mkubwa katika umiliki wa mpira, utengenezaji wa nafasi na umaliziaji, huku Macau ikishindwa kabisa kuhimili kasi ya wapinzani wao.

Ushindi huo ni sehemu ya maandalizi ya Taifa Stars kuelekea mashindano yajayo ya kimataifa.

Mashindano ya FIFA Series yamekuwa yakitoa fursa kwa timu mbalimbali duniani kucheza mechi za kirafiki za ushindani, zikiwasaidia makocha kupima vikosi vyao na kuimarisha mbinu.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.