Beki wa kimataifa wa Uingereza, Harry Maguire, anatarajiwa kuongeza mkataba wake wa kuendelea kuitumikia Manchester United kufuatia mazungumzo yaliyoripotiwa kufikia hatua za mwisho kati yake na klabu hiyo ya Ligi Kuu England.
Taarifa kutoka vyanzo vya karibu na klabu hiyo zinaeleza kuwa pande zote mbili zinaonesha utayari wa kuendelea na ushirikiano, huku uongozi wa United ukiridhishwa na kiwango cha mchezaji huyo katika kipindi cha hivi karibuni.
Inaelezwa kuwa mkataba unaopendekezwa unaweza kuwa wa mwaka mmoja hadi Juni 2027, ukiwa na kipengele cha kuongeza mwaka mwingine kulingana na makubaliano yatakayofikiwa.
Hatua hiyo inakuja wakati ambapo mustakabali wa beki huyo ulikuwa ukizua maswali, hasa baada ya kupoteza nafasi ya kudumu katika kikosi cha kwanza katika vipindi vilivyopita.
Hata hivyo, Maguire ameonesha kurejea katika kiwango chake, jambo lililomfanya kurejea kwenye mipango ya benchi la ufundi na kuwa sehemu muhimu ya kikosi katika mechi za hivi karibuni.
Kwa mujibu wa wachambuzi wa soka, uzoefu wa mchezaji huyo pamoja na uwezo wake wa uongozi ndani ya uwanja ni miongoni mwa sababu zinazochangia klabu hiyo kutaka kuendelea kubaki naye.