Kocha Msaidizi wa Simba Suleiman Matola amesema maandalizi kuelekea mchezo wa ligi kuu dhidi ya Coastal Union yamekamilika na wana matumaini makubwa ya kushinda mchezo huo.
Akizungumza katika mkutano na wanahabari mapema leo, Matola alisema wanatambua ugumu wa mchezo ulio mbele yao hasa kutokana na ubora wa wapinzani wao ambao mara nyingi wamewapa changamoto kila walipokutana.
Matola amesema wamewafuatilia wapinzani wao na kubaini ubora na udhaifu wao ambao watakwenda kuutumia siku ya kesho katika mchezo utakaopigwa uwanja wa Isamuhyo.
"Mechi dhidi ya Coastal Union huwa inakuwa ngumu, katika kuthibitisha hilo mchezo w mzunguuko wa kwanza msimu uliopita uliisha kwa sare"
"Ila tumeangalia mazuri na mapungufu yao ili kuwazidi na kuibuka na ushindi hapo kesho"
"Lengo letu ni kuwa bora dhidi yao katika mchezo huo na hatimaye kuweza kuondoka na alama zote tatu," alisema Matola
Nae Kocha Mkuu wa Coastal Union Mohamed Omary Muya amesema amekiandaa kikosi chake kukabiliana na Simba huku wakilenga kushinda mchezo huo.
Muya amesema anatambua ubora wa klabu ya Simba hivyo wanahitaji kucheza kwa tahadhari huku wakiongeza ufanisi kwenye matumizi ya nafasi

"Tunatambua uwezo wa Simba lakini tumekuja kupambana kutafuta Alama Tatu muhimu. Wachezaji wetu wako vizuri kwenye utimamu wa Mwili kuelekea Mchezo wa Kesho"
"Tumekuwa tukitengeneza nafasi nyingi kwenye mechi zetu lakini hatuzitumii vyema, tumefanya kazi kubwa kwenye uwanja wa mazoezi ili kuhakikisha kesho tunaweza kutumia vyema nafasi. Kama wachezaji wetu wakifuata maelekezo vizuri natumai mashabiki wa Coastal Union watafuraho kesho, " alisema Muya
Simba na Coastal Union zitachuana kesho Alhamisi, April 02 katika mchezo utakaopigwa uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo jijini Dar es salaam



