Klabu ya Yanga imepata faraja baada ya mshambuliaji wake tegemeo, Prince Dube kurejea rasmi kikosini kufuatia kupona majeraha yaliyokuwa yakimsumbua kwa kipindi cha hivi karibuni.
Dube amerejea leo akianza mazoezi pamoja na wachezaji wenzake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Tanzania Prisons utakaopigwa Jumamosi, Aprili 4, 2026 katika Uwanja wa KMC Complex.
Urejeo wa Dube ni habari njema kwa benchi la ufundi la Yanga, hasa katika kipindi hiki ambacho timu inapambana kuendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi. Yanga iliwakosa washambuliaji wake wote tegemeo Dube na Depu katika mechi za mwisho kabla ya mapumziko ya kalenda ya FIFA kutokana na majeraha.
Mbali na Dube, Yanga pia imepokea habari njema ya kurejea kwa nyota wengine waliokuwa majeruhi ambao sasa wameanza mazoezi. Wachezaji hao ni pamoja na Depu, Chadrack Boka, Edmund John na Ibrahim Hamad maarufu kama 'Bacca'.
Yanga waingia kambini Avic Town
Katika hatua nyingine, kikosi cha Yanga kimeingia rasmi kambini Avic Town kukamilisha maandalizi ya mchezo dhidi ya Tanzania Prisons
Awali, timu hiyo ilikuwa ikifanya mazoezi yake katika Uwanja wa KMC Complex, wakati maboresho ya miundombinu yalipokuwa yakifanyika katika kambi ya Avic Town.