Ouma alia na safu ya ushambuliaji Singida BS

Joel JJ By Joel JJ • 3rd April 2026


Ouma alia na safu ya ushambuliaji Singida BS

Kocha msaidizi wa Singida Black Stars david Ouma ameweka wazi kutoridhishwa kwake na safu ya ushambuliaji ya timu hiyo kufuatia mwendelezo wa matokeo yasiyoridhisha katika michezo ya hivi karibuni ya Ligi Kuu.

Akizungumza baada ya mchezo wao wa karibuni waliopoteza dhidi ya Azam Fc wakifungwa mabao 2-1 kwenye uwanja wao wa nyumbani, Ouma alisema changamoto kubwa si namna timu inavyocheza, bali ni kushindwa kutumia ipasavyo nafasi za kufunga mabao wanazozipata ndani ya dakika 90.

Alieleza kuwa kikosi chake kinauwezo wa kumiliki mpira na kutengeneza nafasi nyingi, lakini umakini mdogo wa washambuliaji mbele ya lango umekuwa ukiigharimu timu hiyo kupata matokeo chanya.

“Tunacheza vizuri na tunafika mbele ya lango la wapinzani mara nyingi, lakini hatumalizii nafasi tunazozipata. Hapo ndipo tunapopoteza mechi,” alisema kocha huyo Mkenya

Katika mchezo huo, Singida Black Stars walionekana kuwa na mwanzo mzuri, lakini walishindwa kuendeleza makali yao huku Azam Fc wakitumia vyema nafasi chache walizopata kufunga mabao yaliyoamua matokeo ya mchezo.

Takwimu za Singida BS zinaonyesha kuwa imekuwa ikitengeneza nafasi nyingi za kufunga, lakini kiwango cha ubadilishaji wa nafasi hizo kuwa mabao kimekuwa cha chini, jambo linaloibua maswali kuhusu ufanisi wa safu ya ushambuliaji.

Baadhi ya washambuliaji waliokuwa wakitegemewa kufanya vizuri msimu huu Joseph Gueye Elvis Rupia wameonekana kupoteza makali yao, huku wengine wakishindwa kabisa kuonyesha mchango mkubwa licha ya kupewa nafasi ya kucheza mara kwa mara.

Kutokana na hali hiyo, Ouma amesea benchi la ufundi limeanza kutafuta suluhisho la haraka ili kuboresha safu hiyo kabla ya ratiba ngumu ya michezo ijayo, ikiwa ni pamoja na kuongeza mazoezi maalum ya kumalizia nafasi.

Kocha huyo alisisitiza kuwa bado wana imani na wachezaji waliopo, lakini ni lazima wajitathmini na kuongeza juhudi ili kurejesha ushindani wa timu hiyo katika ligi.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.