Yanga vs Prisons; Makocha wafunguka maandalizi

Joel JJ By Joel JJ β€’ 3rd April 2026


Yanga vs Prisons; Makocha wafunguka maandalizi

Kocha Msaidizi wa Yanga Mathew Silva amesema maandalizi kuelekea mchezo wa ligi kuu dhidi ya Tanzania Prisons yamekwenda vizuri na matarajio yao ni kushinda mchezo huo utakaopigwa kesho Jumamosi, April 04 katika uwanja wa KMC Complex.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari mapema leo, Mathew alisema timu imepata muda wa kujiandaa na mchezo huo huku wachezaji wao wakirejesha utimamu wa miili yao baada ya kipindi kigumu cha mechi mfululizo.

Mathew amesema wamejiandaa kwenda kukabiliana na mechi ngumu dhidi ya Tanzania Prisons ambayo imeonyesha kuimarika katika kila mechi.

"Tumetumia vyema kipindi cha mapumziko ya kalenda ya FIFA kujiimarisha na sasa tunaona tuko tayari kwa mechi inayokuja mbele yetu dhidi ya Tanzania Prisons"

"Tunajuma tunakwenda kukutana na mpinzani mgumu. Ukiangalia katika mechi nne zilizopita, licha ya Tanzania Prisons kutoshinda mchezo wowote, wameonyesha kuimarika," alisema Mathew

Mathew amewashukuru mashabiki wa Yanga kwa kuendelea kuiunga mkono timu yao katika mazingira yote huku akiwataka wajitokeze kwa wingi kwenye mchezo huo utakaopigwa saa 12 jioni.

"Natarajia kuona wananchi wakija kwa wingi uwanjani. Sio tu kuja kwa wingi, wanapaswa kushangilia ili kuipa timu hamasa. Shabiki ni nguzo muhimu kwa timu yoyote inayotafuta matokeo, nisiwe mchoyo wa fadhila kwani mashabiki wa Yanga wamekuwa nasi bega kwa bega kila tulipowahitaji. Tunafahamu mashabiki wetu wa nyumbani wanayo hamu kubwa ya kutuona,” alisema

Nae Kocha Mkuu wa Tanzania Prisons Chadrack Nsajigwa amesema wamejiandaa vyema kuelekea mchezo dhidi ya Yanga ambao wanatarajia hautakuwa mwepesi.

Nsajigwa amewataka mashabiki wa timu hiyo waendelee kuwaunga mkono katika mapambano yao ya kujinusuru na hatari ya kuteremka daraja

"Tuna mechi ngumu, nafasi tuliyopo sio nzuri kwa timu kama Tanzania Prisons kwa hiyo tunajitahidi kufanya kazi kwa bidii ili tuweze kutoka hapa tulipo."

"Tunawaomba mashabiki wetu waendelee kutusapoti kwa hiki tunachokifanya, waendelee kuwasapoti wachezaji na uongozi wa ujumla ili timu iweze kufikia malengo kwa sababu tumekuwa chini mda mrefu"

"Kama tutaendeleza morali tuliyoonyesha katika mechi mbili zilizopita pamoja na sapoti ya mashabiki wetu, nafikiri tunaweza kutoka hapa tulipo," alisema Nsajigwa ambaye amewahi kuwa nahodha wa Yanga na timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars'.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.