Dodoma Jiji, Mbeya City zatakata ligi kuu, Fountain, KMC mambo magumu

Joel JJ By Joel JJ • 3rd April 2026


Dodoma Jiji, Mbeya City zatakata ligi kuu, Fountain, KMC mambo magumu

Timu ya Dodoma Jiji imepanda hadi nafasi ya saba katika msimamo wa NBC Premier League baada ya kuibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Fountain Gate katika mchezo uliochezwa Ijumaa uwanja wa Airtel, Singoda.

Katika mchezo huo uliotawaliwa na Dodoma Jiji, Augustino Nsata aliifungia timu yake bao la kwanza dakika ya 36, ikifuatiwa na Idd Kipagwile kuongeza la pili dakika ya 69. Kassim Mgaza alihitimisha karamu ya mabao kwa kufunga bao la tatu dakika ya nyongeza 90+2, akihakikishia timu yake pointi tatu muhimu.

Ushindi huo umeifanya Dodoma Jiji kufikisha alama 24 na kupanda hadi nafasi ya saba, hatua inayowaweka kwenye eneo salama la msimamo wa ligi, huku Fountain Gate wakishuka hadi nafasi ya 13 na presha ya kushuka daraja ikianza kuonekana wazi.

Katika pambano lingine lililosisimua, Mbeya City iliibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya KMC. Riphat Msuya alifunga bao la kwanza dakika ya 65, akifuatwa na Adilly Buha kufunga penalti dakika ya 77, huku Said Naushad akimalizia ushindi kwa kufunga bao la tatu dakika ya 87.

KMC walijibu kwa mabao ya Paul Adam dakika ya 45 na Adam Uledi dakika ya 79, lakini hawakuweza kuudhibiti ushindi wa Mbeya City. Ushindi huu umewasogeza Mbeya City hadi nafasi ya 12 na kufikisha alama 16, wakati KMC wanaendelea kuburuza mkia wa ligi, jambo linaloongeza presha kubwa ya kupambana na hatari ya kushuka daraja.

Matokeo ya michezo hiyo miwili yamezidi kuongeza ushindani katika ligi hiyo, hususan kwa timu zilizopo katikati ya jedwali pamoja na zile zinazopambana kujinusuru kushuka daraja. 


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.