Rage aishauri Simba iachane na shauri la Damaro

Joel JJ By Joel JJ • 4th April 2026


Rage aishauri Simba iachane na shauri la Damaro

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Simba SC, Ismail Aden Rage, ameishauri klabu hiyo kuachana na sakata la kiungo wa Yanga, Mohamed Damaro Camara, akisema kuendelea kulifuatilia ni kupoteza muda na nguvu bila sababu ya msingi.

Rage alitoa kauli hiyo yakiwa ni maoni yake akisisitiza kuwa hakuna faida kwa Simba kuendelea kushinikiza suala hilo baada ya uamuzi uliotolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kulimaliza.

“Mimi nawashauri viongozi wangu waachane na jambo hili, linatupotezea muda tu, hata tukienda CAS hatuwezi kushinda hivyo ni bora tukijikite kwenye mambo ya msingi yenye manufaa kwa klabu yetu,” alinukuliwa Rage akieleza.

Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya TFF, kupitia kamati yake husika, kutoa uamuzi wa kutupilia mbali malalamiko ya Simba yaliyokuwa yanahoji uhalali wa usajili wa Damaro.

Katika uamuzi huo uliotolewa Aprili 2, 2026, TFF ilieleza kuwa hakukuwa na ukiukwaji wowote wa kanuni za usajili, hivyo kumruhusu mchezaji huyo kuendelea kuitumikia Yanga bila kikwazo.

Awali, Simba walikuwa wamewasilisha malalamiko wakidai kuwa Yanga walikiuka kanuni kwa kuzidisha idadi ya wachezaji wa kigeni, hoja ambayo ilipingwa na kutupiliwa mbali baada ya uchunguzi.

Pamoja na uamuzi huo, taarifa zinaeleza kuwa Simba walikuwa wakifikiria kupeleka suala hilo katika Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS), hatua ambayo Rage ameionya kuwa inaweza isibadili uamuzi wa TFF zaidi ni kupoteza muda na fedha.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.