Makocha wa timu za Simba SC na Coastal Union wamezungumza kuelekea mchezo wa nusu fainali ya Kombe la CRDB utakaopigwa Jumamosi, Juni 20 katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid, mkoani Arusha, huku kila upande ukionesha kujiamini na maandalizi makini.
SIMBA YAAHIDI MAPAMBANO MAKALI NUSU FAINALI
Kocha Mkuu wa Simba, Steve Barker, amesema kikosi chake kipo tayari kwa mtihani huo mgumu dhidi ya Coastal Union, akisisitiza kuwa wamejipanga kuhakikisha wanatinga hatua ya fainali ya mashindano hayo ya taifa.
Barker alisema Simba inatambua ubora wa mpinzani wao, lakini maandalizi yao yamejikita katika kuhakikisha wanapata matokeo chanya.
“Tumejiandaa vyema na tupo tayari kwa mchezo huu wa nusu fainali Kombe la CRDB. Tunatambua ubora na ugumu wa Coastal Union. Mara ya mwisho tulipokutana nao Mkwakwani tulilazimika kutoka nyuma kupata ushindi,” alisema Barker.
Aliongeza kuwa kikosi chake kiko tayari kuonesha kiwango bora zaidi ili kufanikisha lengo la kufika fainali.

COASTAL UNION: TUNAHESHIMU SIMBA, LAKINI TUNAPAMBANA
Kwa upande mwingine, Kocha Mkuu wa Coastal Union, Fikiri Elias, amesema mchezo huo ni wa mtoano na si wa ligi, hivyo kila kitu kinaweza kutokea uwanjani.
Amesema timu yake imejipanga kimkakati na inajua ugumu wa mchezo huo, lakini inalenga kufanya vizuri na kufuzu fainali.
“Tunakwenda kushiriki mchezo wa mtoano na si ligi kuu, lazima mmoja apite kwenda fainali. Tumejipanga vizuri kimbinu, ingawa tunajua mchezo utakuwa mgumu sana,” alisema Elias.
Ameongeza kuwa historia ya mechi zilizopita dhidi ya Simba imekuwa fundisho kwao, na sasa wamejipanga kuonesha tofauti uwanjani.
“Historia ipo ili tujifunze, tumejifunza kwenye michezo iliyopita tuliyocheza dhidi ya Simba, kesho ndio mtaona tulichojifunza,” alisisitiza.



