Timu ya Taifa ya Canada imepata pigo kubwa baada ya kiungo wake nyota, Ismael Koné (24), kupata majeraha mabaya yatakayomuweka nje ya uwanja kwa takribani miezi sita.
Koné alipata majeraha hayo baada ya kuchezewa rafu mbaya na kiungo wa Qatar, Assim Madibo, katika mchezo wa Kombe la Dunia uliochezwa usiku wa kuamkia leo.
Kwa mujibu wa taarifa za awali kutoka kwa madaktari wa timu, mchezaji huyo amevunjika mifupa ya tibia na fibula, ambayo ni mifupa muhimu inayounganisha goti na kifundo cha mguu. Kutokana na ukubwa wa majeraha hayo, Koné anatarajiwa kufanyiwa upasuaji kabla ya kuanza safari yake ya kupona.
Licha ya tukio hilo la kusikitisha, Canada iliendelea kuonyesha kiwango bora uwanjani. Dakika 10 tu baada ya Koné kutolewa nje kwa majeraha, kiungo aliyeingia kuchukua nafasi yake, Nathan Saliba, aliifungia Canada bao la nne.
Saliba aliwagusa mashabiki wengi kwa namna alivyosherehekea bao hilo, ambapo aliinua juu jezi namba 8 ya Koné kama ishara ya kumuunga mkono mwenzake aliyepata majeraha.
Hata hivyo, majonzi ya kuumia kwa Koné hayakuzuia Canada kuandika historia. Ushindi wao wa mabao 6-0 uliwapa furaha kubwa ya kupata ushindi wao wa kwanza wa kihistoria katika Kombe la Dunia 2026.



