Morocco yaizamisha Scotland, yabeba matumaini ya Afrika

Joel JJ By Joel JJ β€’ 20th June 2026


Morocco yaizamisha Scotland, yabeba matumaini ya Afrika

Timu ya taifa ya Morocco imejiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kuibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Scotland katika mchezo wa Kundi C uliochezwa mjini Boston, Marekani.

Ushindi huo umeifanya Morocco kusogea nafasi ya pili kundi hilo nyuma ya vinara Brazil na kuongeza matumaini ya kufanya vizuri kama ilivyofanya katika Kombe la Dunia la mwaka 2022.

Shujaa wa mchezo huo alikuwa kiungo mshambuliaji Ismael Saibari aliyefunga bao pekee la mechi ndani ya sekunde 71 tangu kipenga cha kuanza kilipopulizwa. Bao hilo limekuwa la haraka zaidi kufungwa katika mashindano ya Kombe la Dunia 2026 hadi sasa. Saibari alitumia mwanya katika safu ya ulinzi ya Scotland na kumshinda kipa Angus Gunn kwa shuti kali lililowapa Atlas Lions mwanzo mzuri wa mchezo.

Baada ya kupata bao la mapema, Morocco ilionyesha ubora mkubwa wa kiufundi na kutawala sehemu kubwa ya mchezo. Takwimu zinaonyesha timu hiyo ilifanya zaidi ya pasi 600, idadi kubwa zaidi kuwahi kufanywa na timu ya Afrika katika mechi ya Kombe la Dunia tangu mwaka 1966. Morocco pia ilitengeneza nafasi kadhaa za kuongeza mabao lakini ilishindwa kuzitumia ipasavyo.

Scotland ilionekana kushtushwa na bao hilo la mapema na ilihangaika kupata mpangilio wake katika kipindi cha kwanza. Hata hivyo, kipindi cha pili kilishuhudia timu hiyo ikirejea kwa nguvu na kujaribu kusawazisha. Nahodha Andy Robertson pamoja na Scott McTominay waliongoza mashambulizi ya Scotland, lakini walikwama mbele ya safu imara ya ulinzi wa Morocco iliyoongozwa na Achraf Hakimi na kipa Yassine Bounou.

Dakika za mwisho za mchezo zilikuwa za presha kubwa huku Scotland ikidai kupatiwa penalti kufuatia tukio lililomhusisha McTominay ndani ya eneo la hatari. Hata hivyo, mwamuzi pamoja na VAR hawakuona sababu ya kutoa mkwaju huo, jambo lililozua mjadala mkubwa miongoni mwa mashabiki na wachambuzi wa soka.

Ushindi huo unaifanya Morocco kufikisha pointi nne baada ya kutoka sare ya mabao 1-1 dhidi ya Brazil katika mchezo wake wa kwanza. Kwa upande wa Scotland, waliobaki na pointi tatu baada ya ushindi wao dhidi ya Haiti, sasa wanakabiliwa na mtihani mgumu dhidi ya Brazil katika mchezo wa mwisho wa makundi.

Kocha wa Morocco Mohamed Ouahbi alisifu nidhamu na kiwango cha juu kilichoonyeshwa na kikosi chake, huku kocha wa Scotland Steve Clarke akisema timu yake lazima ijipange upya haraka kabla ya kukutana na Brazil.


  

More Stories

Nyota Paraguay amekula umeme kwa kuziba mdomo
Nyota Paraguay amekula umeme kwa kuziba mdomo
Today, READ MORE β†’
Kivuli cha Camara kinavyomtesa Kassali Simba
Kivuli cha Camara kinavyomtesa Kassali Simba
Today, READ MORE β†’
Brazil yatinga kileleni kundi C baada ya kuichapa Haiti 3-0
Brazil yatinga kileleni kundi C baada ya kuichapa Haiti 3-0
Today, READ MORE β†’
Morocco yaizamisha Scotland, yabeba matumaini ya Afrika
Morocco yaizamisha Scotland, yabeba matumaini ya Afrika
Today, READ MORE β†’
Mutale na Simba wafikia makubaliano ya kuvunja mkataba
Mutale na Simba wafikia makubaliano ya kuvunja mkataba
Today, READ MORE β†’
Pacome afunguka changamoto ya majeraha, atoa ahadi kwa Wananchi
Pacome afunguka changamoto ya majeraha, atoa ahadi kwa Wananchi
Today, READ MORE β†’
Himid aongeza mwaka Azam Fc
Himid aongeza mwaka Azam Fc
Today, READ MORE β†’
Kone kuuguza majeraha kwa miezi 6
Kone kuuguza majeraha kwa miezi 6
Today, READ MORE β†’
Makocha Simba, Coastal Union wafunguka maandalizi nusu fainali CRDB Cup
Makocha Simba, Coastal Union wafunguka maandalizi nusu fainali CRDB Cup
Yesterday, READ MORE β†’
Ni Wikiendi ya kusaka wanafainali CRDB Cup
Ni Wikiendi ya kusaka wanafainali CRDB Cup
Yesterday, READ MORE β†’