Ndoto za Tunisia katika Kombe la Dunia 2026 zimefikia tamati kwa njia ya kusikitisha baada ya kupokea kichapo cha mabao 4-0 kutoka kwa Japan katika mchezo wa Kundi F uliochezwa leo Jumapili Juni 21.
Matokeo hayo yameiacha Tunisia mkiani mwa kundi hilo huku ikipoteza mechi yake ya pili mfululizo, baada ya awali kufungwa mabao 5-1 na Sweden. Kipigo cha Japan kimeifanya timu hiyo kuruhusu mabao tisa katika mechi mbili, jambo linaloonyesha udhaifu mkubwa wa safu yao ya ulinzi.
Japan ilianza mchezo kwa kasi kubwa na kutawala umiliki wa mpira tangu dakika za mwanzo. Mashambulizi ya mara kwa mara yaliwalazimisha Watunisia kucheza muda mwingi katika eneo lao la hatari huku safu ya ulinzi ikionekana kuzidiwa na kasi na mbinu za wapinzani wao.
Daichi Kamada alifunga bao la kwanza dakika ya nne huku Ayase Ueda akifunga mabao mawili na Junya Ito akifunga bao la nne. Tunisia ilijaribu kujibu kupitia mipira ya kushtukiza lakini ilishindwa kuunda nafasi za kutosha za kuisumbua safu ya ulinzi ya Japan.
Kipigo hicho kinaifanya Japan kuimarisha nafasi yake ya kufuzu hatua ya 16 bora huku Tunisia ikibaki bila pointi yoyote baada ya michezo miwili.
Mashabiki wa Tunisia walionekana kuvunjika moyo baada ya kipenga cha mwisho huku wengi wakiamini timu yao haikuonyesha kiwango kinachostahili katika mashindano hayo makubwa. Kuaga kwa namna hii kunakuwa pigo kubwa kwa taifa hilo ambalo lilikuwa na matumaini ya kufanya vizuri zaidi katika michuano ya mwaka huu.
Tunisia hawakuwa wameruhusu bao lolote kwenye hatua ya kufuzu ambapo katika mechi 10, walishinda tisa na kutoka droo mchezo mmoja. Hata hivyo sasa wamepigwa mabao 9 kwenye mechi mbili tu



