Azam FC imefanikiwa kutinga fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB Bank baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Yanga SC katika mchezo wa nusu fainali uliochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza na kudumu kwa dakika 120.
Mchezo huo ulikuwa wa kusisimua kutoka mwanzo hadi mwisho huku ukishuhudia mabingwa watetezi Yanga wakiondolewa kwenye michuano hiyo baada ya kutawala kwa miaka minne mfululizo.
Azam FC walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia Himid Mao aliyefunga kwa kichwa kufuatia uzembe wa mabeki wa Yanga kushindwa kuondoa hatari ndani ya eneo la penalti. Bao hilo liliwapa Azam FC uongozi wa 1-0 hadi mapumziko.
Kipindi cha pili Yanga walirejea kwa nguvu na kufanikiwa kusawazisha kupitia mshambuliaji Prince Dube aliyemalizia kwa kichwa krosi safi ya Allan Okello.
Hata hivyo, makosa ya safu ya ulinzi ya Yanga yaliendelea kuwagharimu baada ya Lameck Lawi kuifungia Azam FC bao la pili dakika ya 85 kwa kichwa akimalizia mpira wa kona uliopigwa na Feisal Salum.
Dakika tatu baadaye, nahodha wa Yanga Bakari Nondo Mwamnyeto aliwarejesha mchezoni Wananchi kwa kufunga bao la kusawazisha kwa kichwa akitumia tena krosi ya Allan Okello na kufanya matokeo kuwa 2-2.
Matokeo hayo yalipeleka mchezo katika dakika 30 za nyongeza ambapo Yanga walionekana kuwa na nafasi kubwa ya kushinda hasa baada ya Azam FC kubaki na wachezaji 10 kufuatia beki Yoro Diaby kutolewa kwa kadi nyekundu kwa kumuangusha Prince Dube akiwa katika nafasi ya wazi ya kufunga.
Licha ya Yanga kushambulia mara kwa mara, kipa wa Azam FC Zuberi Foba alikuwa mwiba kwa kufanya saves muhimu zilizoendelea kuiweka timu yake salama.
Dakika za mwisho za muda wa nyongeza zilileta pigo kubwa kwa Yanga baada ya beki Bacca kufanya kosa la pasi ya kurudisha nyuma. Mshambuliaji Japhet Kitambala aliuwahi mpira huo na kufunga bao la ushindi lililoihakikishia Azam FC tiketi ya fainali kwa ushindi wa mabao 3-2.
Kwa ushindi huo, Azam FC sasa itakutana na Simba SC katika fainali ya CRDB Federation Cup, mchezo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kati ya vigogo hao wa soka la Tanzania. Simba SC walikuwa tayari wamekata tiketi ya fainali baada ya kushinda nusu fainali yao dhidi ya Coastal Union.
Kwa upande wa Yanga, ndoto ya kutetea taji lao imefikia mwisho baada ya kutwaa kombe hilo kwa misimu minne mfululizo. Sasa Wananchi wataelekeza nguvu zao katika mbio za kutetea ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Yanga na Azam FC wanatarajiwa kukutana tena Jumatano ijayo kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar katika mchezo muhimu wa Ligi Kuu ambao unaweza kuwa na athari kubwa kwenye mbio za ubingwa.



