Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga, Ally Kamwe mara baada ya kuwasili Zanzibar, amesema kikosi hicho kimewasili Zanzibar kikiwa na lengo moja tu la kuhakikisha kinatwaa taji la NBC Premier League na kufuta maumivu ya kupoteza mbele ya Azam FC kwenye nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB Bank.
Akizungumza baada ya kuwasili visiwani humo, Kamwe alisema Azam FC wamebaki na simulizi pekee baada ya ushindi wao wa hivi karibuni, huku akisisitiza kuwa Yanga ipo tayari kumalizia kazi kwenye mchezo ujao.
"Tumeshakula ng'ombe mzima, mkiatu ni kidogo sana na pagumu mno," alisema Kamwe akimaanisha kuwa hatua iliyobaki kuelekea ubingwa si kubwa ukilinganisha na kazi ambayo tayari wameifanya msimu mzima.
Hata hivyo, Yanga inakabiliwa na mtihani mgumu mbele ya Azam FC ambao tayari wameonyesha uwezo wao wa kuwazuia Wananchi baada ya ushindi wa mabao 3-2 katika nusu fainali ya Kombe la Shirikisho. Swali kubwa kwa sasa ni je, Azam FC wataweza kuibuka washindi kwa mara ya pili mfululizo dhidi ya Yanga katika Uwanja wa New Amaan Complex, au Wananchi watatumia mchezo huo kuthibitisha ubora wao na kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara?



