Klabu ya Simba SC leo imekutana na waandishi wa habari katika mkutano rasmi kuelekea mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar utakaochezwa kesho saa 10:00 jioni katika Uwanja wa Jamhuri. Mchezo huo unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku timu zote zikiwa na malengo muhimu katika hatua hii ya msimu.
Akizungumza na wanahabari, Kocha Mkuu wa Simba, Steve Barker, amesema maandalizi ya kikosi chake yamekamilika na wachezaji wako katika hali nzuri kuelekea pambano hilo. Barker amesisitiza kuwa lengo kubwa la timu yake ni kuhakikisha wanapata ushindi ili kuendelea kutimiza malengo waliyojiwekea msimu huu.
“Maandalizi kwa upande wetu yapo vizuri kuhakikisha tunashinda mchezo huu muhimu kwetu. Tunafahamu tunakwenda kucheza na timu inayopambana kujiweka katika mazingira mazuri kwenye msimamo wa ligi, hivyo tunatarajia mchezo mgumu lakini tuko tayari,” alisema Barker.
Kwa upande wake, beki wa Simba Nickson Kibabage amesema wachezaji wote wanaelewa uzito wa mchezo huo na umuhimu wa kupata alama tatu. Ameeleza kuwa kikosi kizima kimejipanga kufuata maelekezo ya benchi la ufundi ili kuhakikisha kinaondoka uwanjani na ushindi.
“Wachezaji wote tunafahamu umuhimu wa mchezo huu na tutaingia kwa umakini mkubwa kwa kufuata maelekezo ya benchi la ufundi ili kupata matokeo ya ushindi kama malengo yetu yalivyo,” amesema Kibabage.
Simba wanaingia katika mchezo huo wakihitaji kuendeleza matokeo mazuri huku Mtibwa Sugar nao wakisaka pointi muhimu za kuboresha nafasi yao kwenye msimamo wa ligi. Hivyo, mashabiki wanatarajia kushuhudia pambano kali na la kuvutia katika Uwanja wa Jamhuri kesho jioni.



