Klabu ya Simba SC inatajwa kuanza harakati za kusaka mbadala wa mshambuliaji Jonathan Sowah huku wakielekeza nguvu zao kwa nyota wa Stade Malien ya Mali, Taddeus Nkeng.
Taarifa kutoka duru za usajili, zimebainisha kuwa Simba tayari wako kwenye mazungumzo ya awali kwa ajili ya huduma za mshambuliaji huyo raia wa Cameroon mwenye umri wa miaka 26.
Nkeng alikuwa mmoja wa washambuliaji waliovutia zaidi katika michuano ya Ligi ya Mabingwa (CAFCL) msimu uliopita.
Hata hivyo, Nkeng bado ana mkataba wa mwaka mmoja na Stade Malien, jambo linalomaanisha Simba italazimika kufikia makubaliano na klabu hiyo ya Mali ili kuvunja mkataba wake kabla ya kumleta Msimbazi.
Chanzo cha karibu na mazungumzo hayo kinaeleza kuwa mabosi wa Simba wanaendelea kushinikiza dili hilo likamilike mapema kabla ya kuanza kwa maandalizi ya msimu mpya.
Msimu uliopita, Nkeng alionyesha uwezo wake mkubwa katika CAF Champions League ambapo alifunga mabao manne katika mechi tano za awali za mashindano hayo, akijitangaza kama mmoja wa washambuliaji hatari kutoka Afrika Magharibi. Pia aliifunga Simba katika hatua ya makundi ya michuano hiyo alipokuwa akiitumikia Stade Malien.
Mbali na mafanikio yake nchini Mali, Nkeng ana wasifu wa kuvutia baada ya kupitia akademi ya FC Porto, kucheza nchini Finland akiwa na HJK Helsinki pamoja na Klubi 04, kabla ya kuhamia Venezuela na baadaye kutua Stade Malien.
Simba wanaamini Nkeng anaweza kuziba pengo litakaloachwa na Sowah kutokana na uwezo wake wa kufunga mabao, nguvu za mwili na uzoefu wa kucheza mashindano ya kimataifa. Uongozi wa klabu hiyo unaonekana kutaka kuongeza makali ya safu ya ushambuliaji kuelekea kampeni za Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya CAF msimu ujao.



