Afisa Habari wa Yanga Ali Kamwe, ameibua mjadala mkubwa katika ulimwengu wa soka Tanzania baada ya kutangaza wazi kuwa Yanga watakuwa upande wa Azam FC kwenye Fainali ya CRDB Bank Federation Cup dhidi ya Simba SC.
Kamwe alitoa kauli hiyo wakati wa kikao cha waandishi wa habari baada ya mchezo wa Ligi Kuu uliowakutanisha Yanga na Azam FC visiwani Zanzibar. Licha ya ushindani uliopo kati ya klabu hizo mbili, msemaji huyo alisema Yanga hawatasita kuisapoti Azam katika mchezo wa fainali dhidi ya watani wao wa jadi, Simba.
Akimgeukia Afisa Habari wa Azam FC, Thabit Zakaria (Zakazakazi ) mbele ya waandishi wa habari, Kamwe alisema: “Zakazakazi, tupo pamoja fainali. Weka hapa Kitambala, hapa Ngita, wote kwa pamoja.”
Kauli hiyo ilizua vicheko, makofi na mjadala mkubwa miongoni mwa waandishi wa habari pamoja na mashabiki wa soka waliofuatilia tukio hilo, wengi wakitafsiri maneno hayo kama ishara ya wazi ya Yanga kutamani kuona Azam wakizuia Simba kutwaa taji hilo.
Azam FC walitinga fainali baada ya kuiondoa Yanga kwa ushindi wa mabao 3-2 katika mchezo wa nusu fainali uliochezwa jijini Mwanza, huku Simba SC wakihakikisha nafasi yao kwa kuifunga Coastal Union na kuweka miadi ya kukutana na Wanalambalamba Julai 4, 2026.
Fainali hiyo sasa inatarajiwa kuwa moja ya mechi zenye hisia kali zaidi msimu huu, huku Azam wakisaka taji muhimu na Simba wakitaka kuongeza kombe jingine. Kauli ya Ali Kamwe imeongeza moto wa mchezo huo mapema, na kufanya mashabiki wa soka nchini kusubiri kwa hamu kubwa pambano hilo la Julai 4 mwaka huu .



