Klabu ya Yanga SC imeanza rasmi harakati za kumrejesha kiungo mshambuliaji wake wa zamani, Stephane Aziz Ki, kutoka klabu ya Al Ittihad, imefahamika.
Kwa mujibu wa taarifa, Yanga SC tayari imetuma ofa rasmi kwa Al Ittihad ikiwa ni sehemu ya mpango wa kumrudisha nyota huyo ambaye aliwahi kuwa MVP wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2023/24 kabla ya kutimkia Morocco kujiunga na Wydad CA.
Aziz Ki kwa sasa yupo nchini kwa mapumziko baada ya kumaliza majukumu yake ya msimu nchini Libya, huku taarifa zikieleza kuwa mustakabali wake katika klabu hiyo ya Afrika Kaskazini bado hauko wazi.
Inaelezwa kuwa kiungo huyo raia wa Burkina Faso amekuwa na wasiwasi kuhusu mazingira ya kiusalama nchini Libya, jambo ambalo limechangia kufikiria uwezekano wa kurejea nchini, ambako aliwahi kufurahia mafanikio makubwa akiwa na Yanga SC.
Aidha, Aziz Ki anatajwa kutaka kuwa karibu zaidi na familia yake, hali inayoongeza uwezekano wa kuachana na Al Ittihad mapema kuliko ilivyotarajiwa.
Wakati Yanga SC ikiwa tayari imewasilisha ofa yake, bado mazungumzo kati ya klabu hizo mbili yanaendelea. Ikiwa makubaliano hayatofikiwa, inaelezwa kuwa mchezaji huyo anaweza kufungua shauri katika shirikisho la soka duniani FIFA akidai kutokamilika kwa baadhi ya malipo ya usajili kutoka kwa klabu yake ya sasa.
Kwa hali ilivyo, mashabiki wa Yanga SC wana kila sababu ya kuwa na matumaini, kwani uwezekano wa kumrejesha Aziz Ki Jangwani unaonekana kuwa mkubwa zaidi endapo mazungumzo yataenda vizuri.



