Timu ya Taifa ya Senegal itashuka dimbani leo dhidi ya Iraq katika mchezo wa mwisho wa Kundi I wa Kombe la Dunia 2026, ikiwa na lengo la lazima la kupata ushindi ili kuendelea kuwa na matumaini ya kufuzu hatua ya 32 bora.
Senegal imepoteza michezo yake miwili ya mwanzo, ikianza kwa kichapo cha mabao 3-1 dhidi ya Ufaransa kabla ya kufungwa 3-2 na Norway. Matokeo hayo yameifanya timu hiyo kubaki mkiani mwa kundi, huku ushindi pekee dhidi ya Iraq ukiwa tumaini lao la mwisho la kusalia kwenye mashindano.
Akizungumza kabla ya mchezo huo, Kocha Mkuu Pope Thiaw amesema kikosi chake kimejifunza kutokana na makosa yaliyofanyika katika michezo iliyopita na kipo tayari kupambana. Thiaw amesisitiza kuwa kila kitu bado kinawezekana siku ya mwisho ya hatua ya makundi, mradi wachezaji wake wataonyesha kiwango bora uwanjani.
Senegal itamtegemea mshambuliaji Ismaila Sarr, ambaye tayari amefunga mabao mawili katika mashindano hayo, pamoja na nahodha Kalidou Koulibaly na nyota Sadio ManΓ©, huku kukiwa na uwezekano wa Iliman Ndiaye kupewa nafasi kubwa zaidi. Hata hivyo, kipa Edouard Mendy anatarajiwa kuukosa mchezo huo kutokana na majeraha ya goti.
Kwa upande wa Iraq, nao wamepoteza michezo yao yote miwili baada ya kufungwa 4-1 na Norway na 3-0 dhidi ya Ufaransa. Hali hiyo inaifanya timu hiyo pia kuingia uwanjani ikihitaji ushindi mkubwa, huku ikitegemea matokeo ya michezo mingine ili kubaki na nafasi ya kusonga mbele.
Mchezo huo utakaochezwa katika Uwanja wa BMO Field mjini Toronto unatarajiwa kuwa wa ushindani mkubwa, huku Senegal wakisaka ushindi wa kwanza katika mashindano hayo na kuokoa safari yao ya Kombe la Dunia. Matokeo ya pambano hilo yataamua ikiwa mabingwa hao wa zamani wa Afrika wataendelea kuota ndoto ya kutwaa taji la dunia au wataaga mapema michuano hiyo.



