Aliyekuwa Rais wa Wydad Athletic ya Morocco, Said Naciri, amehukumiwa kifungo cha miaka 10 jela baada ya kupatikana na hatia katika kesi kubwa ya kimataifa ya usafirishaji wa dawa za kulevya iliyotikisa taifa hilo.
Mahakama Kuu ya Morocco ilimtia hatiani Naciri kufuatia uchunguzi uliohusisha mtandao unaojulikana kama "Escobar of the Sahara", ambao umehusishwa na mfanyabiashara wa dawa za kulevya kutoka Mali, Ahmed Ben Brahim, anayehudumia kifungo cha miaka 10 jela nchini humo.
Mbali na kifungo cha miaka 10 gerezani, mahakama pia imemwamuru Naciri kulipa faini ya Dirham milioni 5 za Morocco, sawa na takribani Shilingi bilioni 1.4 za Tanzania.
Mashtaka yaliyomkabili
Naciri alikuwa akikabiliwa na mashtaka kadhaa mazito, yakiwemo:
Utakatishaji wa fedha.
Kushiriki katika mtandao wa usafirishaji wa dawa za kulevya.
Kughushi nyaraka rasmi.
Kutengeneza na kutumia hundi feki.
Matumizi mabaya ya madaraka.
Ufisadi na vitendo vingine vya uhalifu wa kifedha.
Uchunguzi ulivyoanza
Kesi hiyo ilianza mwishoni mwa mwaka 2023 baada ya Ahmed Ben Brahim, kuwataja Naciri pamoja na viongozi wengine wa kisiasa kama washirika wake katika mtandao wa usafirishaji wa dawa za kulevya.
Baada ya kauli hizo, mamlaka za Morocco zilianzisha uchunguzi mkubwa uliowahusisha zaidi ya watu 25, huku viongozi kadhaa wa kisiasa na wafanyabiashara wakifikishwa mahakamani.
Aliwahi kukanusha tuhuma
Katika hatua za awali za kesi hiyo, Naciri alikanusha vikali tuhuma zote zilizokuwa zikimkabili na kudai alikuwa na ushahidi wa kuthibitisha kutokuwa na hatia. Hata hivyo, baada ya mchakato mrefu wa mahakama, amepatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miaka 10 jela pamoja na faini kubwa.
Hukumu hiyo ni miongoni mwa kesi kubwa zaidi kuwahi kuhusisha viongozi wa kisiasa na michezo nchini Morocco, na imeibua mjadala mpana kuhusu mapambano dhidi ya rushwa na uhalifu wa kimataifa nchini humo.



