Mvutano umeibuka ndani ya kambi ya Uruguay kuelekea mchezo muhimu wa Kombe la Dunia 2026 dhidi ya Hispania. Taarifa zinaeleza kuwa baadhi ya wachezaji wakiongozwa na Federico Valverde wameanza kuhoji mbinu za kocha Marcelo Bielsa, huku wakitaka timu ibadili mfumo wa uchezaji katika mechi ijayo.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wachezaji wanaamini mazoezi ya Bielsa yamekuwa makali kupita kiasi na yamechangia kuongezeka kwa majeraha ndani ya kikosi. Pia wanapendekeza Uruguay icheze kwa mfumo wa kujilinda zaidi (low block) dhidi ya Hispania na kutegemea mashambulizi ya kushtukiza badala ya kushambulia muda mwingi.
Ripoti zinaeleza kuwa baada ya malalamiko hayo, Bielsa aliitisha kikao cha timu nzima kilichodumu kwa dakika 48. Inadaiwa kocha huyo alizungumza kwa muda wote huku akiangalia chini, akiwashutumu baadhi ya wachezaji kwa madai ya kujaribu kumfanya afukuzwe kazi.
Hali hiyo imeongeza sintofahamu ndani ya kambi ya Uruguay wakati timu ikijiandaa kwa moja ya mechi zake muhimu zaidi kwenye hatua ya makundi. Hata hivyo, bado hakuna tamko rasmi kutoka Shirikisho la Soka la Uruguay au Marcelo Bielsa kuthibitisha taarifa hizo.
Iwapo taarifa hizi zitathibitishwa, Uruguay italazimika kuweka tofauti zao pembeni haraka iwezekanavyo, kwani mchezo dhidi ya Hispania unaweza kuwa wa kuamua hatma yao katika Kombe la Dunia 2026.



