Kiungo mkabaji na nahodha wa timu ya taifa ya Uganda, Khalid Aucho, anatajwa kuwa kwenye mazungumzo na klabu ya Singida Black Stars kuhusu kusitisha mkataba wake, licha ya mkataba huo kutarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu wa 2026/27.
Taarifa kutoka chanzo cha uhakika imebainisha kuwa pande zote mbili zimeanza majadiliano ya kufikia makubaliano ya kuvunja mkataba huo kwa maridhiano.
Aucho alijiunga na Singida Black Stars msimu uliopita akitokea Yanga SC, baada ya kumaliza kipindi cha mafanikio cha misimu mitatu akiwa Jangwani. Hata hivyo, maisha yake ndani ya Singida BS hayajawa rahisi.
Kiungo huyo amekumbwa na majeraha ya mara kwa mara yaliyomfanya kukosa mechi nyingi za timu yake. Mbali na changamoto za majeraha, aliwahi pia kusimamishwa na klabu kutokana na tuhuma za utovu wa nidhamu kabla ya kurejeshwa kikosini.
Katika kipindi chake akiwa Yanga, Aucho alikuwa mmoja wa wachezaji muhimu waliochangia mafanikio makubwa ya klabu hiyo katika mashindano ya ndani na kimataifa, kiwango kilichomfanya kuwa miongoni mwa viungo bora katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Tetesi zimedokeza kuwa Aucho huenda akarejea klabu yake ya zamani Gor Mahia ya Kenya



